1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kenya: Makundi ya vijana yaungana dhidi ya uhalifu

Wakio Mbogho26 Februari 2021

Zaidi ya makundi 30 ya vijana yaliyosajiliwa nchini Kenya yameungana kuunda vuguvugu la pamoja kwa lengo la  kuwaimarisha kiuchumi na kuwashawishi vijana wenzao kuachana na kujihusisha na matendo ya uhalifu.

https://p.dw.com/p/3py48
 Ndarugu Fluss Müllbeseitigung
Picha: DW/W. Mbogho

Hatua hii inajiri huku kukiwa na ripoti ya kuongezeka kwa uhalifu unaofanywa na vijana katika taifa hilo lenye uchumi mkubwa Afrika Mashariki.

Maafisa wa polisi wanaendelea na uchunguzi baada ya kuwatia mbaroni wasichana 10 wa shule ya upili ya Kirobon ilioko Kaunti ya Nakuru kwa tuhuma za kutumia dawa za kulevya. Joseph Tanui, kamanda wa polisi wa eneo hili amethibitisha kisa hicho.

"Mmoja alikuwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza na wengine ni wa kidato cha nne. Mwalimu mkuu wa shule hiyo Ruth Mwangi aliripoti kwamba aliwapata na bangi shuleni. Polisi walienda shuleni humo na kuwakamata wasichana hao 10. Wamepelekwa hospitalini watakapopimwa na kugundulika iwapo walitumia dawa hizo, uchunguzi unapoendelea.” Amesema Joseph Tanui.

Ni kati ya visa vya uhalifu vinavyoibuka nchini, maafisa wa usalama wakielezea ongezeko la matukio ya matumizi na biashara haramu ya mihadharati, wizi wa kimabavu, visa vya ubakaji na mauaji.

Mwandishi wa habari wa DW Faiz Musa (kulia) akiwashirikisha baadhi ya vijana kwenye mjadala.
Mwandishi wa habari wa DW Faiz Musa (kulia) akiwashirikisha baadhi ya vijana kwenye mjadala.Picha: DW/F. Musa


Katika uzinduzi wa kile kinachoitwa Vuguvugu la Maendeleo kwa Vijana, umoja unaoyaleta pamoja zaidi ya makundi 30 ya vijana, Victor Korir, mwenyekiti wa vuguvugu hilo ameeleza kwamba vijana wanapitia changamoto nyingi zinazowapelekea kugeukia uhalifu wanapokata tamaa maishani. Amesema lengo la mradi huu ni kuwaimarisha vijana, kwa kutambua vipaji, uwezo na mvuto wao, na kisha kuwapa mwongozo na usaidizi wanaohitaji.


Vuguvugu hili linawajumuisha vijana waliorekebisha tabia zao baada ya kujihusisha na uhalifu, na ambao sasa wanahimizwa kutumika katika kuchangia maendeleo. Akiupongeza mradi wenyewe, Thomas Too, Meneja katika afisi ya Mbunge wa eneo la Njoro anautaja kama unaotoa fursa ya kuwafuatilia na kuwaongoza vijana kwani vijana wengi nchini wana ndoto nzuri ila wanakosa mwelekeo na ustahimilivu:
 

Vijana waliojiunga na vuguvugu hili watapokea mafunzo na usaidizi wa kifedha kuendeleza miradi yao. Miradi inayoangaziwa ni pamoja na ujasiriamali, sekta ya afya, mazingira, kilimo cha biashara na elimu ya umma.