1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIran

Iran yaidhinisha wagombea sita wa uchaguzi wa urais Juni 28

9 Juni 2024

Iran imewatangaza wagombea sita, wengi wao wa kihafidhina, walioidhinishwa kwa uchaguzi wa Juni 28 kuchukua nafasi ya Rais Ebrahim Raisi, aliyekufa katika ajali ya helikopta.

https://p.dw.com/p/4gqTf
Rais wa zamani wa Iran Mahmoud Ahmadinejad
Rais wa zamani wa Iran Mahmoud Ahmadinejad akipunga mkono baada ya kuandikisha jina lake kama mgombeaji wa uchaguzi wa urais wa Juni 28 katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Tehran, Iran, Jumapili, Juni 2, 2024.Picha: Sobhan Farajvan/Pacific Press/picture alliance

Wagombea hao waliotangazwa na wizara ya mambo ya ndani walichaguliwa kutoka orodha ya watu 80 waliosajiliwa na Baraza la Uongozi lenye ushawishi mkubwa linalosimamia uchaguzi katika jamhuri hiyo ya Kiislamu.

Miongoni mwa walioidhinishwa ni spika wa bunge mhafidhina Mohammad Bagher Ghalibaf na mjumbe wa zamani wa mazungumzo ya nyuklia mwenye msimamo mkali wa kihafidhina Saeed Jalili.

Ni mgombea mmoja tu mwanamageuzi, Massoud Pezeshkian, ambaye ni mbunge anayewakilisha jimbo la Tabriz katika bunge la Iran, aliyeidhinishwa.

Soma pia:  Mshirika wa Khamenei ajisajili kuwania urais Iran

Waziri wa zamani wa mambo ya ndani mhafidhina Mostafa Pourmohammadi pia ameruhusiwa kugombea.

Rais wa zamani mwenye msimamo mkali Mahmoud Ahmadinejad, ambaye alifungiwa kushiriki mbio za urais katika mwaka mwaka wa 2017 na 2021, tena ametupwa nje kwenye orodha hiyo.

Wengine kwenye orodha hiyo ni meya wa Tehran mhafidhina Alireza Zakaani na makamu wa rais wa sasa Amirhossein Ghazizadeh-Hashemi, ambaye ni mhafidhina wa msimamo mkali anayeongoza Wakfu wa Mashahidi.

Katika uchaguzi wa mwaka wa 2021, Baraza la uongozi liliwaondoa kwenye orodha wagombea kadhaa wanamageuzi na wa siasa za wastani kabla ya uchaguzi wa rais ambao ulimuweka madarakani kiongozi aliyekuwa wa msimamo mkali wa kifadhina, Raisi.