1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

"Habari za uongo", kitisho cha uhuru wa vyombo vya habari

Sekione Kitojo
3 Mei 2019

Dunia leo inaadhimisha siku  ya  uhuru wa  vyombo  vya habari huku kukiwa  na  ukiukwaji  mkubwa  wa  uhuru  huo katika mataifa  mengi, hususan barani  Afrika.

https://p.dw.com/p/3Hrmx
Venezuela Symbolbild Pressefreiheit
Picha: Getty Images/AFP/J. Barreto

Ongezeko  kubwa la taarifa za  uongo na  za  kupotosha ni  mada zinazojadiliwa sana katika  siku hii  ya vyombo vya habari. Hata  hivyo wachunguzi wanasema hakuna  bara  ambalo limesalimika  katika  suala  hili. 

Reporter ohne Grenzen Logo
Shirika la waandishi wasio na mipaka linatetea haki za waandishi dunianiPicha: Getty Images/AFP/B. Guay

Ongezeko  la wimbi  la  taarifa  za  uongo na taarifa ambazo  sio  sahihi ni  mada  zinazojadiliwa katika  wiki  ya Uhuru  wa  vyombo  vya  habari  duniani ambayo inaadhimishwa  kwa ngazi ya dunia nchini  Ethiopia, nchi ambayo  ni  mwenyeji wa  tukio  hilo  baada  ya  kuwaacha huru  waandishi  habari  waliofungwa  gerezani  kama sehemu ya  mageuzi  yanayoendelea  nchini  humo. Wakati dunia  inafanya  maadhimisho  ya uhuru  wa  habari, wafanyakazi  wa vyombo  vya  habari  na  wataalamu wameonesha  wasiwasi  wao  na  kujadili  njia  za kupambana  na  taarifa  za  uongo  ambazo  wanasema zimekuwa  "tishio dhidi  ya  demokrasia."

Uhusiano  kati ya  vyombo  vya habari  na  demokrasia ndio  kauli  mbiu kuu  mwaka  huu, ambapo  zaidi  ya matukio 100  yatafanyika  duniani  kote. Siku ya uhuru wa vyombo  vya  habari  mwaka  huu  inafanyika  kwa  mara ya  kwanza  nchini  Ethiopia , nchi  ambayo  imekuwa ikishutumiwa  kwa muda  mrefu  kwa  kuwafunga waandishi  habari  hadi  pale  waziri  mkuu Abiy Ahmed alipoingia  madarakani  Aprili , 2018. Serikali  yake imewaacha  huru   waandishi  kadhaa waliokuwa  kifungoni.

Amnesty International gegen Türkei
Baadhi ya waandishi habari ambao wako kifungoni katika mataifa mbali mbali dunianiPicha: Getty Images/S.Gallup

Kielelezo cha  uhuru wa habari

Katika  taarifa  yake  kuhusu kielelezo cha  Uhuru  wa habari  duniani  shirika  la  waandishi  wasio  na  mipaka RSF, limesema  bara  la  Ulaya  kwa kiasi  kikubwa  ni sehemu  ambayo  uhuru  wa  vyombo  vya  habari unatekelezwa  kwa kiasi  kikubwa. Lakini  pia  ripoti  hiyo imesema  baadhi  ya  waandishi  isiwafanya  wafumbie macho ukweli  kwamba, katika  miaka  ya  hivi  karibuni, bwawa  limevunjika  na  nguzo  hii  ya  demokrasia imeathirika  pakubwa.

Jamal Khashoggi, Daphne Caruana Galizia, Jan Kuciak, mauaji  dhidi yao  ni  miongoni  mwa  mashambulio makubwa  dhidi  ya  uhuru  wa  vyombo  vya  habari  na ishara  ya  matatizo  makubwa, anasema  hivyo  Christophe Deloire wa  kundi  la  waandishi  wasio  na  mipaka.

Karibu mtu  mmoja  kati  ya  wawili  duniani  hawapati taarifa  huru  zinazoripotiwa. Mauaji ya Khashoggi  mjini Istanbul yameonesha kuhusu  matumizi  makubwa  ya nguvu yanayotumiwa  na  baadhi  ya  nchi  dhidi  ya waandishi  habari.

World Press Freedom Day Karikatur
Wachoraji vibonzo nchini Kenya wameonesha mtazamo wao kuhusu uhuru wa vyombo vya habari dunianiPicha: Gado

Waziri  mkuu wa  Hungary Viktor Orban anatumia  mbinu za kutokuwa na uaminifu kwa  faida  zake na  kuelezea madai  ya  'taarifa za  uongo' kuhalalisha  kukataa  kwake kuzungumza na  vyombo  vya  habari  ambavyo  haviungi mkono  chama  chake.

Waziri wa mambo ya kigeni  wa  Uingereza  Jeremy Hunt amewaambia  waandishi  habari  mjini  Addis Ababa kuwa uhuru wa  vyombo  vya  habari sio maadili  ya  mataifa  ya magharibi  ama  kitu cha anasa kwa  mataifa yanayoendelea.