1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ECOWAS kutoiwekea vikwazo Burkina Faso

Saleh Mwanamilongo
3 Februari 2022

Rais wa Ghana, Nana Akufo-Addo amesema mapinduzi ya nchini Mali yamekuwa ni jambo linalojirudia katika nchi za eneo la Afrika magharibi.

https://p.dw.com/p/46Tly
Ghana Accra | Economic Community of West African States | ECOWAS
Picha: IVORY COAST PRESIDENTIAL PRESS SERVICE/REUTERS

Nana Akufo-Addo ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kilele mjini Accra,Ghana kuhusu hali ya mapinduzi kwenye nchi za Mali,Guinea,Burkina Faso na jaribio la mapinduzi la hivi karibuni huko Guinea-BIssau. 

Mapinduzi ya Mali ya Agosti mwaka 2020 yalifuatiwa na mapinduzi ya pili ya kijeshi katika taifa hilo la Afrika Magharibi mwezi Mei mwaka jana, mapinduzi mengine yalijiri nchini Guinea Septemba mwaka jana, mapinduzi nchini Burkina Faso wiki iliyopita, na jaribio la mapinduzi yaliyoshindwa nchini Guinea-Bissau siku ya Jumanne.

''...mapinduzi ya kijeshi ni jambo la kutia wasiwasi''

Rais wa Ghana Nana Akufo-Addo na ambaye ni mwenyekiti wa jumuiya ya Ecowas amesema wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kilele wa marais wa jumiya hiyo kwamba nilazima kwa jumuiya hiyo kushughulikia kwa pamoja  na kwa uhakika hali hiyo hatari kabla haijaharibu eneo lote la Afrika Magharibi.

"Kuzuka upya kwa mapinduzi ya kijeshi katika eneo letu ni jambo la kutia wasiwasi mkubwa. Mageuzi haya yanapinga njia ya kidemokrasia tuliyochagua.Tunatakiwa kusimama kidete kulinda demokrasia na uhuru katika eneo letu.",alisema Nana.

Nana amesema mkutano huo utazingatia tishio kwa eneo hilo ambalo linatokana na uingiliaji kati wa kijeshi nchini Mali na ushawishi wake katika Guinea na Burkina Faso.

Soma pia : Umoja wa Afrika waisimamisha Burkina Faso baada ya mapinduzi

Je, vikwazo ndio suluhisho ?

Marais wa Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi wametarajia vikwazo vipya
Marais wa Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi wametarajia vikwazo vipyaPicha: IVORY COAST PRESIDENTIAL PRESS SERVICE/REUTERS

Jumuiya ya Ecowas ili simamisha kwa muda uanachama wa Mali, Guinea na Burkina Faso na kuziwekea vikewazo Mali na Guinea,vikwazo ambavyo vimeiathiri Mali baada ya viongozi wa kijeshi kushindwa kuandaa uchaguzi mwezi huu wa Februari na kupendekeza kusalia madaraka hadi mwaka 2025.

Jana Jumatano Mali ilishindwa kulipa zaidi ya dola milioni 31 za malipo ya dhamana kufuatia vikwazo vya kiuchumi iliowekewa na jumuiya ya Ecowas.

Lakini Jumuiya hiyo yenye wanachama 15 pamoja na washirika wake wa nchi za Magharibi hawana niya ya kuongeza msaada kwa utawala wa kijeshi,ambao kwa kiasi kikubwa hauna uwezo wa kudhibiti uasi wa makundi ya kiislamu.

Soma pia :Maelfu waandamana Mali kuunga mkono jeshi na kupinga vikwazo 

Ujumbe wa ECOWAS nchini Burkina Faso

Ujumbe wa Jumuiya ya ECOWAS ulitumwa nchini Burkina Faso Jumatatu kukutana na kiongozi wa mapinduzi Luteni Kanali Paul-Henri Damiba, ambaye alijitangaza kuwa mkuu wa nchi na bado hajatoa pendekezo lolote la ratiba ya kurejesha nchi hiyo katika utawala wa kikatiba.Ujumbe huo ulitarajiwa kutoa taarifa kuhusu mazungumzo hayo kwa wanachama wengine wa ECOWAS kwenye mkutano wa leo Alhamisi.