1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dortmund yamtimua kocha wake Favre

Josephat Charo
13 Desemba 2020

Kibarua cha kocha mkuu wa Borussia Dortmund, Lucien Favre, kimeota majani baada ya kunyolewa bila maji na Stuttgart 5-1 katika mechi waliyocheza nyumbani Signal Iduna Park.(12.12.2020)

https://p.dw.com/p/3meVK
BVB | Lucien Favre
Picha: Lars Baron/Getty Images

Lucien Favre amelipa gharama kubwa kwa matokeo mabaya ya Dortmund huku kocha huyo raia wa Uswisi akitimuliwa saa 24 baada ya kupata kipigo cha mbwa koko 5-1 kutoka kwa VfB Stuttgart.

Wachezaji wa Dortmund watafahamishwa kuhusu uamuzi huo wa kuachana na bosi wao mwenye umri wa miaka 63 katika mazoezi kwa mujibu wa ripoti ya gazeti la Bild na jarida la michezo la Kicker.

Kocha msaidizi Edin Terzic atashikilia mikoba kwa muda hadi mwisho wa mwaka huu.

Favre aliteuliwa kuwa kocha msimu wa kiangazi mwaka 2018 lakini licha ya rikodi ya kutoshindwa mechi 15 kuanza kampeni yake ya kwanza Dortmund na kuongoza msimamo wa ligi kwa alama tisa, klabu hiyo ilitetereka na Bayern Munich walifanikiwa kuwapiku na hatimaye kulishinda taji la Bundesliga siku ya mechi ya mwisho ya msimu uliopita.

Na Bayern walijidhirisha kuwa wakali wakati wa athari za janga la corona 2019/20, ingawa Dortmund walimaliza katika nafasi ya pili kwa mara nyingine tena.

Dortmund kwa sasa wako katika nafasi ya tano baada ya kupoteza mechi tatu mfululizo nyumbani wakiwa nyuma ya Wolfsburg katika nafasi ya nne. Mabingwa watetezi Bayern Munich wako kileleni na RB Leipzig wakiwa na alama sawa 24 lakini wakitofautiana kwa magoli.

Favre ameshindwa kulitwaa kombe la shirkisho la Ujerumani, DFB Pokal, kwa Dportmund huku timu yake ikipigwa kumbo nje ya mashindano hayo katika duru ya tatu ya kampeini zote mbili hadi sasa.

(dpa)