1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dk. Mukwege na Murad washinda Tuzo ya Nobel ya Amani

Daniel Gakuba
5 Oktoba 2018

Daktari raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Dennis Mukwege na mwanaharakati kutoka jamii ya Wayazidi, Nadia Murad, wameshinda Tuzo ya Nobel ya Amani, 2018 kwa jitihada zao za kupambana na unyanyasaji wa kingono.

https://p.dw.com/p/36250
Bildkombo, Bildcombo  Dominique Gutekunst Denis Mukwege und Nadia Murad, Friedens-Nobelpreis 2018
Nadia Murad na Dr. Dennis Mukwege, washindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel 2018

 

Tangazo la ushindi wa Dk. Mukwege na Murad wa Tuzo ya Nobel limetolewa na mwenyekiti wa kamati ya tuzo hiyo Berit Reiss-Andersen mjini Oslo muda mchache uliopita. Bi Reiss Andersen amesema wote wawili wamekuwa nembo ya mapambano dhidi ya janga la unyanyasaji wa kingono, ambalo limeenea kutoka mzozo mmoja hadi mwingine, kama vuguvugu la MeeToo lilivyodhihirisha.

''Washindi hawa wawili wametoa mchango mkubwa katika kuumulika na kuupinga uhalifu huo wa kivita. Dennis Mukwege ni mtu aliyejitolea maisha yake kuwasaidia wahanga hao. Nadia Murad ni shahidi anayesimulia unyanyasaji, uliofanywa dhidi yake na dhidi ya wengine.'' Amesema Reiss-Andersen.

Mchango katika kuwafichua wahalifu

Kongo Kinshasa  - Krankenhaus: Panzi Hospital
Dk. Mukwege amejitolea kuwasaidia wanawake waliobakwa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya KongoPicha: picture-alliance/Yonhap/YNA

Mwenyekiti huyo wa kamati ya tuzo ya Nobel, amesema kila mmoja kati ya watu hao, ametoa mchango kwa njia ya kipekee katika kufichua visa vya unyanyasaji wa kingono katika mizozo na vita, na kusaidia kuwatangaza wahusika wa uhalifu huo ili wakawajibishwe kwa matendo yao.

Dk. Mukwege anasifiwa kwa kujitolea maisha yake yote ya utu uzima kuwatibu maelfu ya wahanga wa ubakaji na unyanyasaji mwingine wa kijinsia katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo - hususan eneo la mashariki mwa nchi hiyo, na kuwa sauti ya kuwatetea. Oktoba mwaka 2012, Dk. Mukwege alinusurika jaribio la kumuuwa, ambapo dereva wake alipoteza maisha

Nadia Murad, UN-Sonderbotschafterin für die Würde der Überlebenden von Menschenhandel
Nadia Murad, amekuwa na ujasiri wa kuzungumzia ubakaji aliofanyiwa na wanamgambo wa IS.Picha: picture-alliance/AP Photo/R. Zak

Nadia Murad ni mmoja wa wasichana na wanawake wa kiyazidi wanaokadiriwa kufika 3,000, ambao walibakwa na kufanyiwa unyanyasaji wa kila aina na wanamgambo wa kundi linalojiita Dola la Kiislamu, IS, na amejitokeza kwa ujasiri kuzungumzia madhila yaliyomkuta pamoja na wenzake.

Nembo ya umoja wa kimataifa

Kamati ya Tuzo ya Nobel imesema Mukwege na Nadia wamekuwa alama ya umoja wa kitaifa na kimataifa, katika kupambana na unyanyasaji wa kingono katika maeneo ya mizozo.

Washindi waliotangazwa leo wamechaguliwa kutoka orodha ya watu 216 na mashirika 115, ambayo ilikuwa imewasilishwa mbele ya kamati. Orodha hiyo ni ya pili kwa ukubwa kuwahi kupokewa na kamati hiyo.

Mwandishi: Daniel Gakuba/afpe,dpae

Mhariri: Iddi Ssessanga