1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Wagombea urais wa Republican washiriki mdahalo bila Trump

Lilian Mtono
28 Septemba 2023

Wapinzani wa aliyekuwa rais wa Marekani Donald Trump na wanaoshiriki mdahalo wa pili wa wagombea urais kupitia chama cha Republican wamemkosoa vikali Trump kwa kushindwa kufika kwenye mdahalo huo.

https://p.dw.com/p/4WtBm
Baadhi ya wagombea saba wa urais kupitia chama cha Republican ambao wameshiriki  mdahalo uliowakutanisha wagombea hao
Baadhi ya wagombea saba wa urais kupitia chama cha Republican ambao wameshiriki mdahalo uliowakutanisha wagombea haoPicha: Mark J. Terrill/AP/picture alliance

Seneta wa Florida Ron DeSantis anayejitanabahisha kama mbadala wa Trump amenukuliwa akisema rais huyo wa zamani alipaswa kushiriki ili kuitetea rekodi yake na hasa kutokana na namna serikali yake ilivyochangia kuongeza deni kwa dola trilioni 7.8, na kuchochea mfumuko wa bei unaoshuhudiwa sasa.

Wagombea saba wa chama hicho kikongwe cha Republican wameshiriki mdahalo huo uliofanyika katika Maktaba ya Ronald Reagan huko California.

Wagombea wengine walimpuuza Trump wakati walipokuwa wakijibu swali la kwanza lililohusiana na mgomo wa wafanyakazi wa kiwanda cha kutengeneza magari kilichopo Michigan, ambako Trump alihutibia badala ya kushiriki mdahalo huo.

Mdahalo huo umefanyika katika kipindi muhimu cha kampeni za Republican ikiwa ni chini ya miezi minne kabla ya kuzinduliwa kwa vikao vya uteuzi wa mgombea wa urais.