1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern Munich yashikwa shati , BVB yapanda

Lilian Mtono
16 Septemba 2019

Mabingwa watetezi wa ligi kuu ya kandanda ya Ujerumani Bundesliga Bayern Munich wameshuka hadi nafasi ya tatu ya msimamo wa ligi baada ya kutoka sare ya 1-1 na RB Leipzig.

https://p.dw.com/p/3PgFO
Deutschland RB Leipzig gegen Bayern München
Picha: imago images/opokupix

Ilikuwa ni dakika ya tatu ya mchezo wakati mtupiaji wa magoli asiye na mpinzani Robert Lewandowski alipoutumia vyema udhaifu wa safu ya ulinzi ya RB Leipzig na kuipatia Bayern Munich bao la kuongoza ikiwa ugenini kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Thomas Muller aliyemzidi maarifa mlinzi wa Leipzig, Lukas Klostermann.

Kosa la mlinzi wa Bayern Lucas Hernandez aliyemchezea rafu mshambuliaji wa Leipzig Yussuf Poulsen katika eneo la hatari muda mfupi tu kabla ya mapumziko, lilisababisha penati iliyochongwa na Mswidi Emil Forsberg wa RB Leipzig na kuipatia timu yake bao la kusawazisha na mechi hiyo kumalizika kwa sare ya 1-1.

Matokeo hayo, yanaifanya Bayern kuwa ya tatu ikiwa na pointi 8, ikitanguliwa na Borussia Dortmund yenye pointi 9 na RB Leipzig iliyoko kileleni.

Kwenye uwanja wa Signal Iduna Park, Borussia Dortmund iliutumia vyema uwanja wake wa nyumbani kwa kuwaadhirisha vibaya Bayer Leverkusen walipoicharaza mabao 4-0. Paco Alacer alifungulia mvua ya mabao, huku nahodha Marco Reus, akiifungia timu hiyo mabao mawili. Kwa matokeo hayo, Borussia Dortmund hivi sasa inashika nafasi ya pili, huku Bayer Leverkusen ikiwa nafasi ya 6.

Michezo mingine iliwakutanisha watani wa jadi, FC Cologne dhidi ya Borussia Mochengladbach, iliyoibuka kidedea ugenini kwa kuifunga Koln, 1-0. Augsburg, ilipata ushindi wa nyumbani wa 2-1 dhidi ya Frankfurt, Union Berlin ilishindwa kutamba nyumbani, baada ya kufungwa mabao 2-1 na Werder Bremen, Hertha Berlin ilikubali kichapo cha 2-1 kutoka kwa Mainz na Fortuna Dusseldorf ilitoshana na Wofsburg kwa bao 1-1.