Afrika katika magazeti ya Ujerumani
10 Januari 2020Kölner Stadt-Anzeiger
Mgogoro unaondelea kwenye nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika siyo tena wa vita vya wenyewe kwa wenyewe.Pande zinazohusika na magogoro huo, ikiwa pamoja na maalfu ya wanamgambo wanoungwa mkono na nchi mbambali kama vile Uturuki.Tangu jenerali muasi, Khalifa Haftar na wapiganaji wake walipojaribu kuuteka mji mkuu wa Libya mnamo mwezi wa Aprili mwaka uliopita,
mgogoro wa nchi hiyo ulianza kubadilika kwa kiwango kikubwa. Mji mkuu Tripoli, ndiyo makao makuu ya serikali ya Libya inayotambuliwa na jumuiya ya kimataifa. Gazeti la Kölner Stadt Anzeiger linatilia maanani kwamba Uturuki pia imejiingiza katika mgogoro wa Libya na si kwa sababu za kisiasa tu bali pia kwa sababu ya kukidhi mahitaji yake ya raslimali kama vile ya gesi. Gazeti hilo pia linaarifu kwamba bunge la Uturuki hivi karibuni lilipitisha mswada wa kuiruhusu serikali ya nchi hiyo kupeleka wanajeshi nchini Libya.
Süddeutsche
Mwanamuziki ambaye pia ni mwanasiasa Bobi Wine anayezidi kupata umaarufu wa kisiasa nchini Uganda anawatikisa viongozi wa nchi hiyo na ndiyo sababu alikamatwa tena wiki iliyopita. Bobi Wine anayendelea kufanikiwa katika shughuli za kisiasa kwa sababu anaungwa mkono na vijana wengi wa Uganda. Takriban asilimia 80 ya watu wa nchi hiyo ni wale wenye umri ulio chini ya miaka 35. Katika muziki wake anaimba juu ya umasikini uliowakumba watu wengi na hasa vijana wasiokuwa na ajira nchini Uganda.
Gazeti la Süddeutsche linasema mwanasiasa huyo kijana anawatoa jasho viongozi wa Uganda kwa sababu ametangaza kuwania urais kwa lengo la kumshinda rais Yoweri Musevi aliye madarakani tangu mwaka1986. Gazeti hilo limemnukulu Bobi Wine akisema katika ujumbe wake kwamba atashinda kwenye uchaguzi ujao hapo mwakani.
Frankfurter Allgemeine
Nalo gazeti la Frankfurter Allgemeine wiki hii linatupeleka Tanzania ambako mkasa wa mwandishi habari Erick Kabendera ulitanda kwenye vyombo vya habari. Gazeti hilo linatufahamisha kwamba Mwandishi habari huyo Kabendera alikamatwa na polisi mwezi Julai mwaka uliopita na amefikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya utakatishaji fedha, kukwepa kulipa kodi na pia kujibu mashakta ya kujihusisha na biashara za kihalifu. Kabendera ambaye ametiwa ndani hakuruhusiwa hata kuhudhuria mazishi ya mama yake.
Gazeti la Frankfurter Allgemeina linasema Kabendera ni mwandishi mashuhuri sana nchini Tanzania na kwa hivyo kukamatwa kwake kumetokana na sababu za kisiasa.Gazeti hilo linaeleza zaidi katika makala yake kwamba kesi inayomkabili mwandishi habari huyo imekuwa inaahirishwa mara kwa mara. Na sasa mwandishi huyo yumo katika hali mbaya ya afya. Ana matatizo ya kupumua na pia mguu wake mmoja umekumbwa na kiarusi. Shirika la kutetea haki za binadamu duniani Amnesty International linataka mwandishi huyo aachiwe mara moja.
Ripota wa Frankfurter Allgemeine kutoka Cape Town anasema katika makala yake kwamba serikali ya Tanzania haina msalie katika kupambana na wapinzani. Amelinukulu shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International likisema kukamatwa kwa Kabendera ni mfano mwingine wa kubanwa kwa uhuru wa vyombo vya habari nchini Tanzania, magazeti yanapigwa marufuku na waandishi habari wanatoweka mara kwa mara na wengine wanafungwa jela. Ripota wa gazeti la Frankfurter Allgemeine anasema katika makala yake kwamba habari hizo haziripotiwi kwenye vyombo vya habari vya nchini Tanzania.
die tageszeitung
Gazeti la die tageszeitung linatupeleka Kenya ambako kituo cha kijeshi kinachotumiwa pia na Marekani kilishambuliwa na magaidi wa Al-Shabaab. Gazeti hilo linaeleza.kwamba magaidi wa Al -Shaabab Jumapili ya wiki iliyopita walijaribu kukishambulia kituo cha kijeshi,Camp Simba, kwenye kaunti ya Lamu nchini Kenya ambacho pia kinatumiwa na wanajeshi wa Marekani. Hata hivyo shambulio hilo lilizuiwa na jeshi la Kenya. Jeshi hilo liliropoti kwamba magaidi wanne waliuliwa. Shambulio hilo kwenye kituo hicho cha kijeshi limesababisha wasi wasi nchini Kenya. Kenya inahofia kuingizwa katika migogoro ya kimataifa. Gazeti la die tageszeitung limetilia maanani kwamba magaidi wa al Shabaab wamefanya shambulio hilo siku chache tu baada ya jenerali wa Iran Qassem Soleimani kuuliwa na Marekani.
Vyanzo:/Deutsche Zeitungen