1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 7 wakamatwa Brussels, Paris kwa ugaidi

Mohammed Khelef25 Machi 2016

Msako unaendelea barani Ulaya baada ya mashambulizi ya kigaidi ya Brussels, huku lawama zikiongezeka dhidi ya vyombo vya usalama kushindwa kuyazuwia mashambulizi hayo yaliyouwa watu zaidi ya 30.

https://p.dw.com/p/1IJoH
Msako wa polisi wa Ubelgiji kwenye kitongoji cha Schaarbeek, Brussels.
Msako wa polisi wa Ubelgiji kwenye kitongoji cha Schaarbeek, Brussels.Picha: Getty Images/AFP/N. Maeterlinck

Watu saba wanaoshukiwa kuwa magaidi wamewekwa kizuizini nchini Ubelgiji kwenyewe na Ufaransa hivi leo, katika wakati ambapo vyombo vya usalama barani Ulaya vikikabiliwa na shinikizo kubwa kutokana na namna vinavyokabiliana na makundi ya siasa kali.

Watu sita kati yao walikamatwa baada ya msako mkali mjini Brussels hapo jana, ikiwa ni siku mbili baada ya washambuliaji wa kujitoa muhanga kujiripua kwenye uwanja wa ndege na kituo cha treni na kupelekea vifo vya watu 31, na majeruhi 300.

Nchini Ufaransa nako, polisi wamemkamata mshukiwa mmoja mjini Paris, wakisema alikuwa kwenye hatua za mwisho mwisho za kuandaa mashambulizi ya kigaidi, baada ya kumshika akiwa na vifurushi kadhaa vya miripuko.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Bernard Cazeneuve, anasema mtu huyo ni raia wa Ufaransa na ni sehemu ya mtandao wa kigaidi, ambao unalenga kuishambulia nchi hiyo, ingawa alisema hakuna uhusiano kati yake na mashambulizi ya Brussels.

Mamlaka za usalama Ulaya zalaumiwa

Polisi inasema mtu huyo aliwahi kutiwa hatiani mwezi Julai akiwa mwenyewe hayupo, ambapo yeye na kiongozi wa kundi la kigaidi mjini Paris aitwaye Abdelhamid Aba Aoud, walitajwa kuwa sehemu ya kundi lililopanga kwenda Syria.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ufaransa, Bernard Cazeneuve.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ufaransa, Bernard Cazeneuve.Picha: picture-alliance/AP Photo/G. Vanden Wijngaert

Mjini Brussels, waendesha mashitaka wamethibitisha kuwa Khalid el Bakrawi aliyejiripua kwenye kituo cha treni cha Maalbeek muda mfupi baada ya kaka yake Ibrahim kufanya hivyo hivy kwenye uwanja wa ndege wa Zaventem, alikuwa akitafutwa kwa waranti wa kimataifa kutokana na mashambulizi ya kigaidi yaliyofanyika Paris mwezi Novemba 2015.

Rais Tayyip Erdogan wa Uturuki alisema hapo juzi kuwa mwenyewe Ibrahim alikuwa amekamatwa nchini mwake na kurejeshwa kwao Ubelgiji, pamoja na ripoti kuwa alikuwa "gaidi wa kigeni." Mtandao wa televisheni ya NBC unasema kaka hao wawili walikuwa pia kwenye orodha ya magaidi ya Marekani.

Kamishna wa Mambo ya Ndani wa Umoja wa Ulaya, Dimitris Avramopoulos, alisema hapo jana kuwa mashambulizi ya Brussels hayakuwa jambo la kushangaza, kauli ambayo inaongeza uzito kwenye lawama zinazotolewa dhidi ya mamlaka husika kushindwa kuyazuwia.

Tayari mawaziri wa sheria na mambo ya ndani wa Ubelgiji wameomba kujiuzulu, lakini Waziri Mkuu Charles Michel amekataa maombi yao.

Hayo yakiendelea, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry, amewasili mjini Brussels, kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kuonesha mshikamano wa Marekani kwa Ubelgiji na Ulaya dhidi ya kitisho cha ugaidi.

Marekani ni mshirika muhimu kwa mataifa ya Ulaya, ambapo hushirikiana kwenye kampeni nyingi za kijeshi duniani, hasa kupitia Shirika lao la Kujihami la NATO.

Mwandishi: Mohammed Khelef/dpa/AFP
Mhariri: Yusuf Saumu