1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakimbizi kushiriki katika Olimpiki

4 Machi 2016

Timu ya wakimbizi ambao watashiriki katika mashindano ya mwaka huu ya Olimpiki mwezi Agosti mjini Rio de Janeiro, Brazil huenda ikawajumuisha wanamichezo kumi.

https://p.dw.com/p/1I7Vq
Thomas Bach Präsident Internationales Olympisches Komitee
Picha: picture-alliance/dpa/L. Gillieron

Rais wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki - IOC Thomas Bach amesema timu hiyo ambayo iliidhinishwa rasmi na kamati kuu ya IOC na kupewa jina la Timu ya Olimpiki ya Wanamichezo Wakimbizi, itachaguliwa kutoka kwa kundi la wanamichezo 43 ambao tayari wametambuliwa na IOC na kusaidiwa na fedha za wao kupata mafunzo. "Timu hii itapewa fursa sawa kama za timu nyingine na wanamichezo na kwa kuikaribisha timu ya wanamichezo wakimbizi wa Olimpiki katika mashindano ya Olimpiki ya Rio 2016, tunataka kutuma ujumbe wa matumaini kwa wakimbizi wote duniani. Wanamichezo hawa wakimbizi hawana bendera ya taifa wanaloliwakilisha, hawana bendera ya kutembea nayo kwenye msafara, hawana wimbo wa taifa, hivyo tutawakaribisha wanamichezo hawa wakimbizi katika mashindano ya Olimpiki na bendera ya Olimpiki na wimbo wa Olimpiki".

Maelfu ya wakimbizi, wengi wao kutoka Syria wamevuka mpaka kupitia Uturuki na Ugirikki na kuingia Ulaya.

Kwingineko, Rabat utakuwa mji wa kwanza barani Afrika kuandaa mashindano ya riadha ya kimataifa ya Diamond League, utakapokuwa mwenyeji wa mashindano hayo baadaye mwaka huu. Rabat, mji mkuu wa Morocco, utaandaa mashindano ya tatu ya msimu huu mnamo 22 Mei.

Akitangaza umauzi huo, Rais wa Shirikisho la riadha duniani (IAAF) Sebastian Coe amesema: “Tuna furaha sana kupeleka mashindano haya makuu ya riadha hadi kwenye bara jingine.”

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/reuters
Mhariri: Yusuf Saumu