Vita Iran: Trump awaita washirika wa NATO "waoga"
Imechapishwa 20 Machi 2026ilisahihishwa mwisho 20 Machi 2026
Unachohitaji kujua
Unachotaka kufahamu:
- Trump 'awananga' washirika wa NATO kwa kushindwa kumsaidia vitani
- Walinzi wa Mapinduzi wa Iran wameripoti kwamba msemaji wao ameuliwa katika shambulizi la anga.
- Khamenei asema adui 'ameshindwa' katika ujumbe ulioandikwa wa mwaka mpya wa Nowruz
- Iran yasema itawalenga maafisa wa Marekani na Israel katika 'maeneo ya burudani'
- Kyiv yatuma vikosi vya jeshi Mashariki ya Kati kudhibiti droni za Iran
Khamenei asema adui 'ameshindwa' katika ujumbe ulioandikwa wa mwaka mpya wa Nowruz
Kiongozi mkuu wa Iran Mojtaba Khamenei siku ya Ijumaa alisema maadui wa jamhuri hiyo ya Kiislamu wanashindwa katika vita dhidi ya Marekani na Israel katika ujumbe wa maandishi ulioandikwa kwa ajili ya Mwaka Mpya wa Kiajemi, Nowruz.
"Kwa sasa, kutokana na umoja maalum ambao umeundwa miongoni mwenu wananchi -- licha ya tofauti zote za kidini, kiakili, kitamaduni na kisiasa -- adui ameshindwa," alisema Khamenei, ambaye bado hajaonekana hadharani tangu alipotajwa kumrithi baba yake Ayatollah Ali Khamenei ambaye aliuawa katika shambulizi la anga mwanzoni mwa vita.
Khamenei kwenye taarifa hiyo iliyotolewa kwenye chaneli yake ya Telegram,
alisema kwamba mashambulizi dhidi ya Uturuki na Oman hayakufanywa na Iran au vikosi vyake washirika.
Iran yasema itawalenga maafisa wa Marekani na Israel katika 'maeneo ya burudani'
Msemaji wa jeshi la Iran amesema kwamba Tehran inaweza kuwalenga maafisa na wanajeshi wa Marekani na Israel katika maeneo ya starehe na ya kitalii.
Msemaji wa jeshi, Abolfazl Shekarchi alinukuliwa na shirika la habari la Mehr akisema kwamba Iran inawafuatilia ‘maafisa wa adui, makamanda, marubani na askari,’ na kuongeza kuwa ‘maeneo ya starehe, vivutio vya utalii na vituo vya burudani’ hayatakuwa salama tena.
Marekani na Israel wamewaua maafisa kadhaa wa ngazi ya juu wa Iran kupitia mashambulizi ya angani, akiwemo Kiongozi Mkuu Ali Khamenei na hivi karibuni mkuu wa usalama Ali Larijani.
Mnamo Ijumaa, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi la Kiislamu (IRGC) limesema kwamba msemaji wao, Ali Mohammad Naini aliuliwa katika mashambulizi ya Marekani na Israel.
Trump awaita washirika wa NATO "waoga" kwa kushindwa kusaidia vita vyake na Iran
Rais Donald Trump aliwashambulia washirika wa NATO siku ya Ijumaa kwa kushindwa kumuunga mkono kwenye vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran, akiwaita washirika hao wa muda mrefu wa Marekani kuwa "waoga."
"Bila Marekani, NATO NI KAMA CHUI ASIYE NA MENO!" Trump aliandika katika chapisho kwenye mitandao ya kijamii.
Rais wa Marekani alilalamika kwamba nchi za NATO hazikutaka kujiunga na vita dhidi ya Iran, lakini bado zinalalamika kuhusu bei kubwa za mafuta.
"Sasa kwa kuwa kijeshi, bila hatari kubwa kwao, wanalia kuhusu bei ya juu ya mafuta wanazolazimika kulipa, lakini hawataki kusaidia kufungua Mlango Bahari wa Hormuz, hatua rahisi ya kijeshi ambayo ndiyo sababu kuu ya bei hizo za juu za mafuta. Rahisi sana kwao kufanya, bila hatari kubwa,” aliandika.
“WAOGA, na TUTAKUMBUKA!”
Kyiv yatuma vikosi Mashariki ya Kati kudhibiti droni za Iran — afisa wa ulinzi wa Ukraine”
Ukraine imetuma vikosi vya kijeshi katika nchi kadhaa za Mashariki ya Kati kusaidia kukamata ndege zisizo na rubani, amesema afisa mwandamizi wa ulinzi wa Ukraine, Rustem Umerov.
Katika chapisho kwenye X, Umerov alisema alitembelea Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Saudi Arabia, Qatar na Kuwait, pamoja na Jordan na kwamba Kyiv imetuma vikosi katika nchi hizo.
“Wataalamu wa kijeshi wa Ukraine wanafanya kazi katika kila moja ya nchi hizi chini ya uratibu wa Baraza la Usalama wa Taifa na Ulinzi,” alisema.
“Vikosi vya kukamata droni vimetumwa kulinda miundombinu ya kiraia na ile muhimu. Kazi ya kupanua maeneo ya ulinzi inaendelea.”
Umerov ni katibu wa Baraza la Usalama wa Taifa na Ulinzi la Ukraine, chombo kinachojumuisha Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy, mawaziri kadhaa na maafisa wengine waandamizi.
Jeshi la Ukraine lina uzoefu wa kuangusha droni za Iran aina ya Shahed, ambazo zimekuwa zikitumiwa na Urusi tangu ilipoivamia Ukraine Februari 2022.
Tehran imelenga maeneo katika nchi za Ghuba ya Uajemi kujibu mashambulizi ya mabomu ya Marekani na Israel nchini Iran.
Msemaji wa Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi auawa katika mashambulizi ya Marekani na Israel, Iran yasema
Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi la Kiislamu la Iran (IRGC) kimesema kwamba msemaji wao, Ali Mohammad Naini, ameuliwa katika mashambulizi ya Marekani na Israel, hatua inayoongeza idadi ya vifo vya maafisa wa ngazi ya juu kwenye mzozo huo.
Naini ‘alifariki shahidi katika shambulizi la kigaidi, kikatili na la woga lililofanywa na Marekani na Wazayuni alfajiri,’ Walinzi hao walitangaza kupitia tovuti yao ya Sepah News.
Vyombo vya habari vya serikali ya Iran pia vimeripoti kwamba Naini, ambaye amekuwa msemaji wa IRGC tangu 2024, aliuliwa wakati wa mashambulizi hayo, ingawa bado hakuna uthibitisho wa haraka kutoka Israel au Marekani.
Ufaransa ‘kuendelea na msimamo wake’ kuhusu Ukraine licha ya vita vya Iran — Macron
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema kwamba Paris haitapunguza msaada wake kwa Ukraine baada ya kuzuka kwa vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran.
‘Tunaendelea na msimamo wetu,’ Macron alisema kupitia chapisho kwenye mtandao wa X.
‘Vita nchini Iran havitaifanya Ufaransa kuiacha Ukraine, ambako uvamizi wa Urusi unaendelea.’
Amesema kwamba jeshi la wanamaji la Ufaransa lilikamata meli katika Bahari ya Mediterania iliyoshukiwa kuwa sehemu ya meli ‘kivuli’ za Urusi zinazotumika kukwepa vikwazo vya kimataifa.
Kuwait: Moto wazuka katika kiwanda cha kusafisha mafuta baada ya mashambulizi ya droni za Iran
Kuwait imesema Ijumaa kwamba moto ulizuka katika kiwanda cha kusafisha mafuta cha Mina Al-Ahmadi kufuatia mashambulizi mawili ya ndege zisizo na rubani kutoka Iran.
Imesema kwamba vikosi maalumu vinaendelea kufanya kazi kuudhibiti moto huo.
Kiwanda hicho tayari kilikuwa kimeshambuliwa siku ya Alhamisi katika shambulio la awali lililofanywa na Iran.
Kiwanda hicho kina uwezo wa kusafisha takriban mapipa 730,000 ya mafuta kwa siku.
Tehran imeongeza mashambulizi yake dhidi ya miundombinu ya nishati ya nchi za Ghuba baada ya Israel kushambulia kiwanda cha gesi cha South Pars nchini Iran.
Watu watano wakamatwa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kwa njama za ‘kuhujumu uchumi wa taifa’ kwa maelekezo ya Iran
Mamlaka za Umoja wa Falme za Kiarabu zimesema zimewakamata watu watano wanaoshukiwa kuhusika na mtandao haramu unaohusishwa na Tehran, shirika la habari la serikali WAM liliripoti Ijumaa.
WAM lilisema kwamba vyombo vya usalama vya UAE "vimevunjilia mbali" kile vilichoeleza kuwa ‘mtandao wa kigaidi unaofadhiliwa na kuendeshwa na Hezbollah ya Lebanon na Iran.
Kundi hilo linatuhumiwa kujaribu ‘kuingilia uchumi wa taifa na kutekeleza njama kutoka nje zinazotishia uthabiti wa kifedha wa nchi’ pamoja na ‘kutakatisha pesa, kufadhili ugaidi na kutishia usalama wa taifa.’
Ripoti ilisema mtandao huo uliendesha shughuli zake UAE ‘kwa kivuli cha biashara bandia.