1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaadhimisha miaka 75 ya katiba

23 Mei 2024

Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steimeier amesema katiba ya Ujerumani au sheria ya msingi ilikuwa zawadi iliyokuwa na thamani kubwa, hasa baada ya utawala wa kikatili wa kinazi.

https://p.dw.com/p/4gDTE
Miaka 75 ya katiba ya Ujerumani inayojulikana kama sheria ya msingi
Rais Frank Walter Steinmeier amesema katiba ya Ujerumani inatakiwa kuenziwa, kutunzwa na kulindwa kila siku nchini humo.Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Sheria hiyo ya msingi ilianza kutumika tarehe 23 mwezi Mei mwaka 1949, ambayo pia ni tarehe ya kuanzishwa kwa shirikisho la Ujerumani miaka 35 iliyopita. Rais Frank Walter Steinmeier amesema zawadi hiyo kuu kwa Ujerumani haipaswi tu kukumbukwa, inatakiwa kuenziwa, kutunzwa na kulindwa kila siku nchini Ujerumani. Amesema katiba hiyo imeunda mfumo thabiti unaoleta muingiliano wa amani wa watu katika jamii mbali mbali. 

Bunge la Ujerumani lapitisha sheria kuwatimua majaji wenye misimamo mikali

Akiwa katika maadhimisho ya miaka hiyo 75 ya katiba ya Ujerumani au sheria mama, Steinmeier amesema katiba hiyo ni moja ya katiba kongwe Ujerumani na imekuwa mfano kwa katiba nyengine nyingi. Kiongozi huyo wa Ujerumani amesema sheria hiyo kuu inayoiongoza nchi hadi sasa ndio imekuwa msingi wa uhuru, demokrasia na haki na kuhakikisha utangamano wa watu wa Ujerumani.

Kwa maoni yake katiba iliyoundwa miaka 75 iliyopita ni imara na imeivusha nchi katika migogoro kadhaa pamoja na changamoto chungu nzima.

Vurugu za kisiasa zinahatarisha demokrasia 

Frank-Walter Steinmeier
Rais wa Ujerumani Frank-Walter SteinmeierPicha: picture-alliance/ZUMA Press

Kando na hayo Steinmeier ametahadharisha kwamba mashambulizi ya kisiasa yameanza kushuhudiwa tena nchini Ujerumani akisema ana wasiwasi juu ya ongezelo la mashambulizi dhidi ya wanasiasa wanaokuwa kazini au katika kampeni mbali mbali. Ameongeza kuwa vurugu zinahatarisha demokrasia ya nchi na kusambaratisha misingi yake.

Rais Steinmeier wa Ujerumani, sasa amewatolea mwito wajerumani wote kudumisha utamaduni wa kisiasa inayoendana na na demokrasia.

Serikali ya Ujerumani yadaiwa kukiuka katiba katika kazi zake

Sherehe ya kuadhimisha miaka hiyo imehudhuriwa na viongozi watano wa vyombo vya katiba. Kando na rais mwenyewe alikuwepo pia rais wa bunge la Ujerumani Bundestag Bärbel Bas, rais wa Baraza la juu la bunge la Ujerumani, Manuela Schwesig, rais wa mahakama ya katiba Stephan Harbarth pamoja na Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz.

Baadae wananchi pia watakuwa na nafasi ya kusherehekea katiba yao katika hafla ya demokrasia itakayoandaliwa katika majengo ya serikali ya mjini Berlin kuanzia kesho Ijumaa hadi Jumapili na siku ya Jumamosi katika majengo ya serikali za wilaya mjini Bonn ambapo rais Frank-Walter Steimeier anatarajiwa kufungua makaazi yake mapya mjini humo yaliyopewa jina la  Hammerschmidt.

dpa