Uganda yapiga kura huku jeshi na mtandao vikizua taharuki
15 Januari 2026
Waganda wanajiandaa kupiga kura katika uchaguzi wa rais unaotarajiwa kuendeleza utawala wa muda mrefu wa Rais Yoweri Museveni, huku ukizua hofu kuhusu uwazi wa mchakato, nafasi ya jeshi katika siasa na mustakabali wa demokrasia.
Museveni, aliye madarakani tangu mwaka 1986, anawania muhula wa saba ambao utamkaribisha zaidi kutawala kwa karibu nusu karne. Hata hivyo, anakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa mwanamuziki aliyegeuka mwanasiasa, Bobi Wine, mwenye umri wa miaka 43, anayewakilisha kizazi kinachotamani mabadiliko ya kisiasa.
Mbali na wagombea hawa wawili wakuu, wagombea wengine sita wanashiriki kinyang'anyiro hicho katika taifa lenye takribani watu milioni 45. Tume ya uchaguzi inasema kuna wapiga kura milioni 21.6 waliojiandikisha.
Wachambuzi wengi wanaamini Museveni atabaki madarakani, lakini akiwa na umri wa miaka 81, inadaiwa amekuwa akitegemea zaidi vyombo vya usalama kulinda mamlaka yake. Mwanawe, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ndiye kamanda mkuu wa jeshi, hali inayozua maswali kuhusu kuingiliwa kwa uchaguzi.
Upinzani, hasa Bobi Wine, umelishutumu jeshi kwa kuingilia mchakato wa uchaguzi, madai ambayo serikali imekuwa ikiyakanusha vikali.
Mtandao wazimwa kabla ya kura
Chini ya saa 48 kabla ya kuanza kwa upigaji kura, Tume ya Mawasiliano ya Uganda iliagiza kampuni za mawasiliano kusitisha huduma za intaneti na kusimamisha usajili wa laini mpya za simu.
Serikali ilieleza kuwa hatua hiyo ilikuwa muhimu kudhibiti upotoshaji wa taarifa, udanganyifu wa uchaguzi na vitisho vya kiusalama vinavyoweza kusababisha vurugu.
Hatua hiyo imekosolewa vikali na wanaharakati wa demokrasia, wanaotegemea mtandao kusambaza taarifa za ukiukwaji wa uchaguzi kama vile kuiba kura na kujaza masanduku.
Kwa wapinzani, kuzimwa kwa mtandao ni jaribio la kuzuia uwazi na kuathiri ufuatiliaji wa matokeo ya uchaguzi katika vituo vya kupigia kura.
Mkakati wa "kulinda kura”
Chama cha Bobi Wine, National Unity Platform, kimewahimiza wafuasi wake kubaki karibu na vituo vya kupigia kura baada ya kupiga kura ili kufuatilia zoezi hilo na kuzuia udanganyifu.
Sheria ya Uganda inaruhusu wapiga kura kukusanyika umbali wa mita 20 kutoka kituo cha kupigia kura, lakini maafisa wa uchaguzi wamewataka wapiga kura kuondoka mara baada ya kupiga kura.
Mvutano huu umeibua hofu kwamba hali hiyo inaweza kuchochea vurugu iwapo vikosi vya usalama vitaamua kuwalazimisha wapiga kura kufuata maelekezo ya tume.
Wine amewataka wafuasi wake kutumia simu kurekodi tukio lolote lisilo la kawaida, akisisitiza umuhimu wa ulinzi wa kura.
Wanajeshi mitaani na hofu ya vurugu
Katika hotuba ya mkesha wa Mwaka Mpya, Museveni alisema alishauri vyombo vya usalama kutumia mabomu ya machozi kuvunja mikusanyiko ya kile alichokiita "upinzani wa kihalifu”.
Katika uchaguzi wa mwaka 2021, Wine alikumbwa na vipigo, kukamatwa kwa wafuasi wake na madai ya matumizi makubwa ya nguvu na polisi.
Ameliambia shirika la habari la AP kuwa wafuasi wake wasiopungua watatu waliuawa katika matukio ya kampeni, akidai kuwa jeshi limechukua usimamizi wa uchaguzi.
Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa imeripoti kile ilichokiita "ukandamizaji uliokithiri”, ikiwemo utekaji na kutoweka kwa wafuasi wa upinzani.
Hofu ya urithi wa madaraka
Museveni ameendelea kubaki madarakani kwa kufuta ukomo wa mihula na umri, huku wapinzani wakifungwa au kusukumwa pembeni kisiasa.
Kutokuwepo kwa mrithi anayetambulika ndani ya chama tawala cha National Resistance Movement kumeongeza uzito wa madai kuwa mwanawe, Muhoozi Kainerugaba, anaandaliwa kuchukua uongozi.
Muhoozi amewahi kuibua mabishano kupitia mitandao ya kijamii kwa kauli kali dhidi ya wapinzani, hatua zilizoongeza hofu ya kuanzishwa kwa utawala wa kifamilia nchini Uganda.