1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uganda yapiga kura huku jeshi na mtandao vikizua taharuki

15 Januari 2026

Wakati Uganda ikiingia kwenye uchaguzi wa rais, hatua za kuzima mtandao, kuwepo kwa wanajeshi mitaani na madai ya kuingiliwa kwa mchakato zimeibua maswali mazito kuhusu uwazi wa kura na mustakabali wa demokrasia.

https://p.dw.com/p/56ops
Uganda, Kampala 2026 | Maandalizi ya uchaguzi wa Bunge kwa vifaa vya uchaguzi mjini Kampala
Masanduku yaliyo na vifaa vya uchaguzi yakiwa yamepangwa kabla ya kusambazwa kutoka ghala la Tume ya Uchaguzi ya Uganda, kuelekea uchaguzi mkuu wa nchi hiyo, katika kitongoji cha Ntinda mjini Kampala, Uganda, Januari 8, 2026.Picha: Abubaker Lubowa/REUTERS

Waganda wanajiandaa kupiga kura katika uchaguzi wa rais unaotarajiwa kuendeleza utawala wa muda mrefu wa Rais Yoweri Museveni, huku ukizua hofu kuhusu uwazi wa mchakato, nafasi ya jeshi katika siasa na mustakabali wa demokrasia.

Museveni, aliye madarakani tangu mwaka 1986, anawania muhula wa saba ambao utamkaribisha zaidi kutawala kwa karibu nusu karne. Hata hivyo, anakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa mwanamuziki aliyegeuka mwanasiasa, Bobi Wine, mwenye umri wa miaka 43, anayewakilisha kizazi kinachotamani mabadiliko ya kisiasa.

Mbali na wagombea hawa wawili wakuu, wagombea wengine sita wanashiriki kinyang'anyiro hicho katika taifa lenye takribani watu milioni 45. Tume ya uchaguzi inasema kuna wapiga kura milioni 21.6 waliojiandikisha.

Wachambuzi wengi wanaamini Museveni atabaki madarakani, lakini akiwa na umri wa miaka 81, inadaiwa amekuwa akitegemea zaidi vyombo vya usalama kulinda mamlaka yake. Mwanawe, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ndiye kamanda mkuu wa jeshi, hali inayozua maswali kuhusu kuingiliwa kwa uchaguzi.

Upinzani, hasa Bobi Wine, umelishutumu jeshi kwa kuingilia mchakato wa uchaguzi, madai ambayo serikali imekuwa ikiyakanusha vikali.

Uganda, Mukono 2026 | Polisi wanatumia gesi ya kutoa machozi dhidi ya wafuasi wa Bobi Wine katika mkutano wa kampeni za uchaguzi
Wafuasi wa chama kikuu cha upinzani NUP, wakikumbana na rungu la jeshi la polisi wakati wa kampeni katika Wilaya ya Mukono.Picha: Hajarah Nalwadda/AP Photo/picture alliance

Mtandao wazimwa kabla ya kura

Chini ya saa 48 kabla ya kuanza kwa upigaji kura, Tume ya Mawasiliano ya Uganda iliagiza kampuni za mawasiliano kusitisha huduma za intaneti na kusimamisha usajili wa laini mpya za simu.

Serikali ilieleza kuwa hatua hiyo ilikuwa muhimu kudhibiti upotoshaji wa taarifa, udanganyifu wa uchaguzi na vitisho vya kiusalama vinavyoweza kusababisha vurugu.

Hatua hiyo imekosolewa vikali na wanaharakati wa demokrasia, wanaotegemea mtandao kusambaza taarifa za ukiukwaji wa uchaguzi kama vile kuiba kura na kujaza masanduku.

Kwa wapinzani, kuzimwa kwa mtandao ni jaribio la kuzuia uwazi na kuathiri ufuatiliaji wa matokeo ya uchaguzi katika vituo vya kupigia kura.

Mkakati wa "kulinda kura”

Chama cha Bobi Wine, National Unity Platform, kimewahimiza wafuasi wake kubaki karibu na vituo vya kupigia kura baada ya kupiga kura ili kufuatilia zoezi hilo na kuzuia udanganyifu.

Sheria ya Uganda inaruhusu wapiga kura kukusanyika umbali wa mita 20 kutoka kituo cha kupigia kura, lakini maafisa wa uchaguzi wamewataka wapiga kura kuondoka mara baada ya kupiga kura.

Mvutano huu umeibua hofu kwamba hali hiyo inaweza kuchochea vurugu iwapo vikosi vya usalama vitaamua kuwalazimisha wapiga kura kufuata maelekezo ya tume.

Wine amewataka wafuasi wake kutumia simu kurekodi tukio lolote lisilo la kawaida, akisisitiza umuhimu wa ulinzi wa kura.

Uganda, Kampala 2026 | Hitimisho la kampeni za Rais Yoweri Museveni kabla ya uchaguzi wa Bunge
Rais wa sasa wa Uganda na mgombea urais wa chama cha National Resistance Movement (NRM), Yoweri Museveni, akitoa hotuba wakati wa mkutano wa mwisho wa kampeni za chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa Uganda wa mwaka 2026, uliofanyika Kampala tarehe 13 Januari 2026.Picha: AFP

Wanajeshi mitaani na hofu ya vurugu

Katika hotuba ya mkesha wa Mwaka Mpya, Museveni alisema alishauri vyombo vya usalama kutumia mabomu ya machozi kuvunja mikusanyiko ya kile alichokiita "upinzani wa kihalifu”.

Katika uchaguzi wa mwaka 2021, Wine alikumbwa na vipigo, kukamatwa kwa wafuasi wake na madai ya matumizi makubwa ya nguvu na polisi.

Ameliambia shirika la habari la AP kuwa wafuasi wake wasiopungua watatu waliuawa katika matukio ya kampeni, akidai kuwa jeshi limechukua usimamizi wa uchaguzi.

Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa imeripoti kile ilichokiita "ukandamizaji uliokithiri”, ikiwemo utekaji na kutoweka kwa wafuasi wa upinzani.

Bobi Wine: Hatutavumilia hujuma zozote kwenye uchaguzi

Hofu ya urithi wa madaraka

Museveni ameendelea kubaki madarakani kwa kufuta ukomo wa mihula na umri, huku wapinzani wakifungwa au kusukumwa pembeni kisiasa.

Kutokuwepo kwa mrithi anayetambulika ndani ya chama tawala cha National Resistance Movement kumeongeza uzito wa madai kuwa mwanawe, Muhoozi Kainerugaba, anaandaliwa kuchukua uongozi.

Muhoozi amewahi kuibua mabishano kupitia mitandao ya kijamii kwa kauli kali dhidi ya wapinzani, hatua zilizoongeza hofu ya kuanzishwa kwa utawala wa kifamilia nchini Uganda.