1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya kijeshi ya Niger yavunja mabaraza ya miji

5 Aprili 2024

Mkuu wa serikali ya kijeshi ya Niger, Jenerali Abdourahamane Tiani, ameamuru kuvunjwa kwa mabaraza yote ya miji nchini humo na amemuweka afisa wa jeshi kusimamia mji mkuu, Niamey.

https://p.dw.com/p/4eSJO
Jenerali Abdouramane Tiani, mkuu wa serikali ya kijeshi ya Niger.
Jenerali Abdouramane Tiani, mkuu wa serikali ya kijeshi ya Niger.Picha: ORTN/Télé Sahel/AFP/Getty Images

Kulingana na vyombo vya habari vya serikali, Jenerali Tiani, ambaye alimuondoa madarakani rais wa taifa hilo la Afrika Magharibi katika mapinduzi Julai 2023, alitia saini amri ya kuvunjwa kwa mabaraza ya manispaa na ya majimbo, ambayo yalichaguliwa mara ya mwisho mwaka 2020, bila ya maelezo zaidi.

Soma zaidi: Mtoto wa rais wa zamani wa Niger aachiwa kwa dhamana

Redio ya serikali ilitangaza amri ya pili ya kiongozi huyo iliyohusu majina ya wanajeshi, polisi na maafisa wa umma watakaosimamia serikali za mitaa.

Miongoni mwa viongozi walioondolewa ni meya wa mji mkuu wa Niger, Oumarou Dogari, ambaye nafasi yake imechukuliwa na kanali wa kijeshi.