1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Randrianirina aapishwa kuwa Rais wa Madagascar

17 Oktoba 2025

Kiongozi wa mapinduzi wa Madagascar, Kanali Michael Randrianirina ameapishwa kuwa rais kufuatia maandamano yaliyoongozwa na vijana ambayo yalimlazimisha Rais aliyekuwepo madarakani Andry Rajoelina kulikimbia taifa hilo.

https://p.dw.com/p/52APo
Madagaska Antananarivo 2025 | Kanali Michael Randrianirina anaapishwa kuwa Rais
Mtawala mpya wa kijeshi wa Madagascar, Kanali Michael Randrianirina, akizungumza baada ya kuapishwa kama rais siku ya Ijumaa akichukua nafasi ya Andry Rajoelina kufuatia mapinduzi yaliyomuondoa madarakani, katika mahakama ya kikatiba mjini Antanariv, Madagascar, Oktoba 17, 2025.Picha: Siphiwe Sibeko/REUTERS

Katika hafla iliyofanyika katika Mahakama ya Juu ya Katiba mjini Antananarivo, Kanali Michael Randrianirina amekula kiapo chake akisema:

"Nitatimiza kikamilifu, kwa ukamilifu na kwa haki majukumu makubwa ya nafasi yangu kama Rais wa Jamhuri ya Madagascar." Naapa kwamba nitatekeleza mamlaka niliyopewa na nitatoa nguvu zangu zote kulinda na kuimarisha umoja wa kitaifa na haki za binadamu."

Awali, Randrianirina alitangaza kuwa jeshi limechukua madaraka na kuvunja taasisi zote isipokuwa Bunge la Kitaifa. Alieleza kuwa kamati inayoongozwa na jeshi itatawala kwa kipindi cha hadi miaka miwili sambamba na serikali ya mpito, kabla ya kuandaa uchaguzi mpya.

Maandamano ya Gen Z yachochea mabadiliko ya uongozi

Maandamano ya Madagascar | Jeshi linachukua madaraka
Maandamano ya Madagascar Jeshi linachukua madarakaPicha: Rafalia Henitsoa/Anadolu Agency/imago images

Randrianirina alikuwa kamanda wa kikosi maalum cha CAPSAT, ambacho kilihusika katika mapinduzi ya mwaka 2009 yaliyomleta Andry Rajoelina madarakani. Hata hivyo, wiki iliyopita alijitenga na Rajoelina, akiwahimiza wanajeshi wasiwafyatulie risasi waandamanaji.

Wakati vijana wengi wakishangilia kuanguka kwa utawala wa Rajoelina, baadhi yao wameanza kuonyesha wasiwasi kuhusu kasi ya jeshi katika kujaza nafasi ya uongozi.

Rajoelina, ambaye alikimbilia nje ya nchi mwishoni mwa wiki, aliondolewa madarakani na wabunge, lakini amekataa kujiuzulu licha ya maafisa wengi wa usalama kujiondoa upande wake.

Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika zalaani mapinduzi

Umoja wa Afrika na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, wameyalaani mapinduzi hayo, ambayo yametokea baada ya wiki kadhaa za maandamano ya kizazi cha "Gen Z".

Maandamano hayo, yaliyoanza mwezi uliopita, yanafanana na harakati za vijana wa Gen Z katika Nepal, Sri Lanka na maeneo mengine. Vijana wa Madagascar walianza kuandamana kupinga kukatika mara kwa mara kwa maji na umeme, lakini baadaye wakaanza kuibua masuala mengine kama vile gharama ya maisha, ukosefu wa fursa, na tuhuma za ufisadi na upendeleo miongoni mwa viongozi wa juu.

Madagascar ina idadi ya watu takriban milioni 30, ambapo robo tatu ya watu wanaishi katika umasikini. Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, kati ya mwaka wa uhuru 1960 hadi 2020, pato la taifa kwa kila mtu liliporomoka kwa asilimia 45.