1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa akiri watawa kunyanyaswa kingono

Sylvia Mwehozi
6 Februari 2019

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis amekiri hadharani kashfa ya mapadri na maaskofu kuwanyanyasa kingono watawa ndani ya kanisa hilo, na kuapa kwamba atazidisha juhudi za kupambana na tatizo hilo.

https://p.dw.com/p/3CrHM
Vatikanstadt - Papst Franziskus bei Weihnachtsansprache an Vatikanmitarbeiter
Picha: Reuters/T. Gentile

Papa Francis alikiri uwepo wa tatizo hilo kwa mara ya kwanza wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari wakati akirejea mjini Roma kutoka Falme za Kiarabu. Kukiri huko kunakuja wiki mbili kabla Papa hajafanya mkutano na maaskofu ili kushughulikia kashfa za mapdri wanaowanyanyasa watoto kingono na namna viongozi wakubwa katika kanisa walivyojaribu kuficha uhalifu huo.

Francis aliulizwa kuhusu mapadri kuwanyanyasa wanawake, hususan watawa ambao wamekuwa nguzo katika kanisa hilo hasa kwenye nyanja za elimu, huduma za afya na huduma za kijamii duniani kote, ikiwa atazingatia mwelekeo kama huo kushughulikia suala hilo.

Alisema "sio kwamba kila mmoja anafanya hivi, lakini kumekuwepo na mapadri na maaskofu ambao wanafanya hivi", Francis aliwaeleza waandishi wa habari. "Je tufanye jambo zaidi? ndio! Je tuna dhamira? Ndio. Lakini ni njia ambayo tumeianza", alisema Francis.

Nonnen in der katholischen Kirche
Watawa wa Kanisa Katoliki Picha: Imago/UIG

Suala hilo limeangaziwa mnamo wakati  Kanisa Katoliki likikumbwa na kashfa lukuki za unyanyasaji kingono dhidi ya watoto na ushawishi wa kampeni ya MeToo ambayo imefanya wakiri kuwa watawa wanaweza kuwa wahanga wa unyanyasaji ikiwa kunakosekana usawa katika mahusiano ya madaraka.

Mwaka uliopita shirika la habari la Associated Press pamoja na vyombo vingine vya habari viliripoti kesi kadhaa za unyanyasaji kingono dhidi ya watawa huko India, Afrika, Ulaya na hata Amerika ya Kusini, ushahidi wa kuwa tatizo hilo si la eneo moja.

Mwezi Novemba, shirika linalowakilisha wanawake wa kikatoliki duniani kote, pamoja na shirika la kimataifa la umoja wa taasisi za Kikatoli lilivunja utamaduni wa ukimya na usiri ambao uliwazuia watawa kupaza sauti na kuwataka watawa hao kuripoti unyanyasaji huo kwa wakubwa wao na polisi.

Kukiri kwa Papa juu ya tatizo hilo kunakuja wakati akijiandaa kuamua mustakabali wa kadinali wa zamani wa Kimarekani Theodore McCarrick, anayetuhumiwa kuwadhalilisha watoto pamoja na watu wazima.

China Katholiken zelebrieren Messe zu Ostern
Mapadri na Wakatukumeni huko China baada ya ibadaPicha: picture-alliance/dpa/A. Wong

Francis alibainisha kwamba Papa Benedict XVI alikuwa amechukua hatua dhidi ya padri wa Kifaransa ambaye anadaiwa kuvunja kiapo kwa kuwanyanyasa kingono watawa katika shirika aliloliunda mwenyewe. Kesi hiyo ilitoa mwangaza juu ya suala la unyanyasaji wa uhusiano wa madaraka, na kama kanisa katoliki lilifikiria kuzingatia kuwa waseminari na watawa wako hatarini ukilinganisha na mapadri na maaskofu ambao hudhibiti kila kitu kuanzia likizo, masomo na hata mishahara.

Francis alisema watawa hao walitumika katika "utumwa wa ngono" wakiwa mikononi mwa Kasisi Marie-Dominique Philippe na mapadri wengine. Jumuiya ya St. Jean ilikubali mwaka 2013 kwamba Philippe alizini na wanawake kadhaa kulingana na gazeti la Kifaransa la kanisa Katoliki La Croix.

Phillipe alikufa mwaka 2006. Miaka mitatu baadaye, askofu wa eneo hilo alimsimika mkuu mpya kwenye nyumba ya watawa. Baadhi walimkataa na kumfuata mkuu wa zamani wa kike alipoanzisha taasisi mpya huko Uhispania.

Papa Francis alielezea kwamba unyanyasaji wa mapadri dhidi ya watawa bado unashughulikiwa  kwa msingi wa kesi moja moja.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi

Mhariri: Daniel Gakuba