1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Muuguzi mmoja Ujerumani ahukumiwa kifungo cha maisha

5 Novemba 2025

Mahakama moja mjini Aachen nchini Ujerumani, imemhukumu leo kifungo cha maisha jela muuguzi mmoja kwa mauaji ya wagonjwa 10 na jaribio la kuwaua wengine 27 kwa sindano za sumu.

https://p.dw.com/p/538rR
Muuguzi wa wazee nchini Ujerumani
Muuguzi wa kiume wa kutunza wazee, (kushoto) akimsaidia mwanamke mzee katika nyumba ya wazee huko Stuttgart, kusini-magharibi mwa Ujerumani mnamo Mei 2007Picha: AP

Mahakama hiyo ilimpata mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 44 na hatia ya makosa aliyotenda kati ya Desemba 2023 na Mei 2024 katika hospitali ya Wuerselen karibu na mji wa Aachen.

Waendesha mashtaka wamesema muuguzi huyo aliwachoma sindano ya dozi kubwa za dawa za usingizi au kutuliza maumivu wagonjwa na hasa wazee, kwa lengo la kupunguza majukumu yake wakati wa zamu za usiku.

Muuguzi hakuonyesha kujutia mauaji aliyofanya

Waliiambia mahakama kwamba mwanamume huyo alikuwa na tatizo la kiakili na hakuwahi kuwahurumia wagonjwa na pia hakuonyesha kujutia.

Mwanamume huyo, ambaye hakutajwa jina hadharani, alishtakiwa na waendesha mashtaka kwa kujifanya "bwana wa maisha na kifo" juu ya wale walio chini ya uangalizi wake.

Upande wa utetezi ulitaka kuachiliwa kwake huru katika kesi hiyo iliyoanza Machi.