1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Musk aanza umiliki wa Twitter kwa kufuta kazi wafanyakazi

Tatu Karema
28 Oktoba 2022

Elon Musk, amekamilisha ununuzi wa kampuni ya Twitter na kuwafuta kazi maafisa wakuu. Awali kampuni hiyo ilikataa dau la dola bilioni 44 kuinunua lakini baadaye ilimshtaki Musk alipotangaza mipango ya kuacha ununuzi huo

https://p.dw.com/p/4InTj
USA Twitter Elon Musk
Picha: Adrien Fillon/ZUMA Press Wire/picture alliance

Baada ya Musk kuchukuwa udhibiti wa twitter, amewafuta kazi mkurugenzi wake mkuu Parag Agrawal, afisa mkuu wa fedha, afisa mkuu wa masuala ya sheria na sera za Twitter na mwanasheria mkuu wa kampuni hiyo. Haya yameripotwa Alhamisi na gazeti la New York Times.

Masaa machache baadaye, Musk aliandika ujumbe katika mtandao huo wa twitter akisema "ndege ameachiliwa," akimaanisha nembo ya kampuni hiyo ya Twitter. Pia alichapisha video yake katika mtandao huo iliomuonesha akiingia katika makao makuu ya kampuni hiyo siku ya Jumatano ikiambatana na maneno yaliosema'' Naingia katika makao makuu ya Twitter- Hilo mulitie maanani''

Musk akanusha uvumi wa nia yake ya ununuzi wa twitter

Siku ya Alhamisi, alituma ujumbe ambapo alidai kuwa uvumi kuhusu nia yake ya ununuzi wa kampuni hiyo umekuwa sio sawa na kwamba alikuwa anainunua kampuni hiyo kusaidia ubinadamu.

Siku ya Jumatano, hisa za twitter zilikaribia dau lililtolewa na Musk la dola 53.72 kwa ununuzi  wa kila hisa za mtandao huo. Hiyo ilikuwa ishara kwamba wawekezaji walitarajia kuendelea kwa makubaliano hayo ya dola bilioni 44 kabla ya muda wa mwisho uliowekwa na mahakama ya mji wa Delaware  mwishoni mwa juma.

Logo von Twitter ist auf einem Smartphone
Nembo ya twitter Picha: Thomas Trutschel/photothek/picture alliance

Mapema mwezi Oktoba mahakama ya Delaware iliweka muda huo wa mwisho kufuatia mvutano mkubwa ambapo Musk alitia saini makubaliano hayo ya kununua kampuni ya twitter na baadaye kujaribu kujiondoa. Twitter ilimshtaki na kumlazimisha kuendelea na mkataba huo.

Watumiaji wengi wa Twitter wameelezea wasiwasi wao kuhusu ahadi ya Musk ya kulinda "uhuru wa kujieleza" kwenye mtandao huo ikiwa ni pamoja na kuzingatia kumrejesha Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump katika mtandao huo baada ya kufungiwa akaunti yake kwa kuhusika katika ghasia za Januari 6 katika jengo la bunge la Marekani.

Hii leo, maoni mbali mbali yametolewa kuhusiana na Muss kuchukuwa udhibiti wa twitter.

Umoja wa Ulaya wamuonya Musk kufuata sheria

Thierry Breton, afisa wa Umoja wa Ulaya anayesimamia udhibiti wa mitandao,  amemuonya Musk kwamba kampuni hiyo lazima ifuate sheria za umoja huo barani Ulaya.

Katika kujibu ujumbe wa Musk aliotuma mapema katika mtandao wa twitter, Breton alisema kuwa barani Ulaya, ndege huyo ambaye ni nembo ya twitter atapaa kwa sheria za Umoja wa Ulaya.

Wakati huo huo, mwanzilishi mwenza wa twitter Biz Stone amewashukuru wakuu wa kampuni hiyo waliofutwa kazi kwa mchango wao wa pamoja katika kampuni hiyo.

Steven Beardsley wa kitengo wa biashara cha DW, amesema suala kuu lililobaki kwasasa ni jinsi Musk atakavyotumia mtandao huo wa Twitter.