1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo mwishoni mwa wiki hii

22 Februari 2008

Bundesliga-Munich yaionya Hamburg kuchunga na Chelsea yaweza kutwaa kombe lake la kwanza msimu huu jumapili.

https://p.dw.com/p/DBm3
Bayern munich iko pointi 3 mbele ya Bremen.Picha: AP

Baada ya duru ya kwanza ya champions League-kombe la klabu bingwa barani Ulaya kati ya wiki hii ambamo Bayern munich waliongoza timu 4 za Ujerumani katika kombe la Ulaya la UEFA huku Schalke pekee ikipepea bendera ya Ujerumani katika kombe hilo la klabu bingwa, Munich imepeleka salamu kali kwa Hamburg- mahasimu wao kesho kuwa wembe ulioinyoa Aberdeen kati ya wiki utawanyoa na wao huko Allianz Arena.

Katika Premier League-Ligi ya Uingereza, Manchester united na Arsenal wanarudia tena ubishi wao wa kinyan’ganyiro cha ubingwa wakati Chelsea inaania kombe lake la kwanza msimu huu katika finali ya Kombe la Ligi la FA kati yake na Tottenham.

Nahodha wa Bayern Munich Oliver Kahn, ameionya Hamburg kuwa ichunge kwani Munich sasa imepambamoto ama si hivyo, kesho itakiona kilichomtoa kanga manyoya.

Kahn atakaestaafu kucheza katika Bundesliga baada ya kumalizika msimu huu,amesema kuwa Bayern munich hivi sasa inakaribia kileleni mwa nguvu zake baada ya kuikumta hannover mwishoni mwa wiki iliopita mabao 3:0 na kufungua mwanya wa pointi 3 kati yake na Bremen.Tangu Munich hata Hamburg zina siku 3 tu za kupumua kabla changamoto yao ya kesho.Munich na Hamburg zilishiriki katika mapambano ya kombe la Ulaya la UEFA hapo jumatano huku Hamburg ikimudu suluhu 0:0 na FC zurich wakati Munich iliizaba Aberdeen ya Scotland mabao 5-1.

Kwa kocha wa hamburg –mholanzi Huub Stevemns hii ni nafasi ya mwisho kesho kutamba mbele ya hasimu yake kocha wa Munich Ottmar Hitzfeld .kwani kuanzia Julai mwaka huu,Jürgen klinsmann,aliekua kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani katika kombe la dunia 2006 atachukua mahala pake.Hitzfeld atakua kocha wa timu ya taifa ya Uswisi ambako aliwahi kucheza katika Ligi ya huko.

Leo Bremen iliopo nafasi ya pili ya ngazi ya Ligi nyuma ya Munich ina miadi Eintracht Frankfurt huko Frankfurt.Frankfurt ilizabwa bao 1:0 na Hansa Rostock mwishoni mwa wiki iliopita.

Na baada ya kuitoa FC Porto kwa bao 1:0 mjini Gelsenkirchen ,Schalke 04 iliopo nafasi ya 5 katika ngazi ya Ligi wanaumana na Bayer Leverkusen walioichapa galatasary ya uturuki mabao 5-1 kwenye kombe la UEFA.

Changamoto nyengine za bundesliga ni kati ya Stuttgart na Karlsruhe,Borussia Dortmund na Hansa Rostock na Aremenia Bielefeld wanatembelewa nyumbani na Duisburg.

Kesho kalenda ya Bundesliga mwishoni mwa wiki hii inakamilishwa na mpambano kati ya Nuremberg na Cottbus.

Katika Premier League-ligi ya Uingereza,mabingwa Manchester united na mahasimu wao Arsenal wanarudia ugomvi wao wa kuania taji wakati Chelsea inacheza jioni hii finali ya kombe la ligi la FA.

Arsenal inafunga safari leo kwenda Birmingham wakati Manchester ina miadi leo na Newcastle.Manchester united iliopo nyuma ya Arsenal kwa pointi 5v ilihitaji bao la dakika za mwisho juzi kusawazisha katika mpambano wa champions league na Lyon ya Ufaransa.Chelsea iliomudu suluhu 0:0 na wagiriki Olympiakos juzi ,inatarajiwa leo kulitetea kwa mafanikio kesho kombe la Ligi la FA uwanjani Wembley.

Katika Serie A, Ligi ya Itali, Inter Milan hadi sasa haikushindwa na inaongoza kwa pointi 11 usoni wakifuatwa na AS Roma.Lakini baada ya kuzabwa juzi mabao 2-0 na FC Liverpool ya uingereza katika champions League ,Inter inapaswa kuchunga.

Katika La Liga-ligi ya Spain ,Real Madrid mwishoe inapumua kuweza kucheza katika uwanja wa nyumbani wa Santiago Bernabeu wakiwa na miadi na majirani zao Getafe hapo kersho jumapili.Real ililazwa mara 2 nje ya Madrid.Katika la Liga lakini,Real haikuwahi kulazwa nyumbani Madrid.Barcelona ina miadi kesho na Levante.

Katika Ligi ya Ufaransa Lyon iliozima vishindo vya Manchester United ina miadi na Metz wakati paris Saint germain imnakutana na Monaco.

Mwishoe, Singapore na sio Moscow iliopewa heshima kuandaa michezo ya kwanza ya olimpik kwa vijana –Youth Olympic games mwaka 2010.Singapore yenye wakaazi milioni 4.5 iliushinda mji wa Moscow hapo juzi.

Singapore haikuwahi kuandaa mashindano makuu ya kimataifa lakini IOC-halmashauri kuu ya olimpik ulimwenguni imeona bora kuanzia Singapore kwa michezo ya vijana ya olimpik.