Mtoa misaada Mfaransa akamatwa Jamhuri ya Afrika ya Kati
10 Machi 2026
Mamlaka katika Jamhuri ya Afrika ya Kati zimemkamata mfanyakazi wa misaada wa Ufaransa wa shirika la hisani la Madaktari Wasio na Mipaka (MSF) na kumtuhumu kwa kutishia usalama. Hayo yamesemwa Jumatatu na wizara ya ulinzi.
Tangazo hilo lilitolewa siku nne tu kabla ya mwanadiplomasia mkuu wa Ufaransa Jean-Noel Barrot kufanya ziara ya kwanza huko Bangui kuwahi kufanywa na waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa katika kipindi cha miaka saba. Barrot atakutana na Rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Faustin Archange Touadera siku ya Alhamisi.
Wizara ya ulinzi imesema mfanyakazi huyo wa misaada wa MSF alikamatwa karibu na mji wa kusini mashariki wa Zemio Alhamisi iliyopita na alishukiwa kwa shughuli zinazolenga kuvuruga hali ya usalama katika eneo hilo.
Wizara hiyo ilimtuhumu mshukiwa kwa kuwasiliana na wahalifu na kufanya kazi kwa uchochezi wa uasi miongoni mwa wakazi wa eneo hilo wa kabila la Azande ili kuwageuza kuwa kinyume na mamlaka zilizochaguliwa kisheria nchini humo.
Ilidai kwamba alivuka mpaka kinyume cha sheria na kuingia Jamhuri ya Afrika ya Kati kutoka nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.