1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Malawi bado ina matumaini uwekezaji utaingia nchini humo

Mohamed Dahman13 Agosti 2008

Malawi iko katika harakati za kuongeza uhusiano wake wa kibiashara na pembe tafauti duniani, magharibi na mashariki.

https://p.dw.com/p/Ew3T
Mashamba ya mahindi nchini MalawiPicha: Aliaa Tayea

Nchi hiyo ndogo ya kusini mwa Afrika inatumai uwekezaji wa kigeni utaisaidia nchi hiyo kuwa ya uchumi wenye kuzalisha na kusafirisha nje badala ya kuwa mlaji na muagizaji wa mahitaji yake kutoka nje kama vile ilivyo hivi sasa.

Baraza la Biashara la Jumuiya ya Madola CBC ambalo huunganisha masoko chipukizi katika ulimwengu wa nchi zilizoendelea na sekta binafsi ya kimataifa limekuwa rafiki au mshirika wa hivi karibuni wa Malawi katika harakati zake za kutafuta kampuni za uwekezaji za kigeni zenye kusifiwa sana lakini sio rahisi kupatikana.

Waziri wa Fedha wa Malawi Goodall Gondwe ameliambia baraza hilo kwamba uchumi wa Malawi

ni uchumi mzuri kama uchumi mwengine wowote ule ambao mtu angelipenda kuwekeza na kwamba wamefanikiwa sana kuutuliza uchumi wa nchi hiyo.

Baraza la Biashara la Jumuiya ya Madola CBC na serikali ya Malawi zilikubalina hapo tarehe 18 mwezi wa Julai kwamba baraza hilo litasaidia katika kuvutia wawekazaji kwa viwanda vya nchi hiyo vya madini,utalii,teknoljia ya habari, mawasiliano ya simu,kilimo na usindikaji wa bidhaa za kilimo,uchukuzi ,nishati na huduma za mabenki.

Baraza hilo liliasisiwa na wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Madola katika mkutano wao wa mwaka 1997 ili kutumia mtandao unaoiunganisha Uingereza na makoloni yake ya zamani kuchochea uwekezaji na biashara.

Makubaliano hayo mapya yanakuja kufuatia harakati nyengine za biashara ambapo Malawi imeanzisha na taifa kubwa linaloinukia kiuchumi China kwa lengo la kukuza uhusiano wa biashara kati ya nchi hizo mbili.

Jumla ya mapendekezo 25 ya miradi mikubwa yamewasilishwa kwa CBC na wafanya biashara wa Malawi huku miradi ya mabenki ikipindukia thamani ya dola milioni 10.

Baraza hilo la Jumuiya ya Madola litarahisisha uwekazaji wa dola milioni 20 na timu ya waatalamu wa fedha kutoka nchi zilizoendelea kwa ajili ya kujenga kituo cha kisasa cha mikutano ya kimataifa.

Kupitia taarifa iliosainiwa na Malawi na CBC nchi hyio inategemewa kuendeleza ushirika binafsi wa wananchi kwa ajili ya kifungu cha miundo mbinu ya kiuchumi na kuongeza uzalishaji katika sekta ya kilimo ili kuhakikisha usalama wa chakula.

Kwa muijibu wa waziri wa fedha wa Malawi Goodal Gondwe nchi yake inashawishi wawekezaji kujenga sekta binafsi ya nchi hiyo ambayo amesema ni engine ya ukuaji wa uchumi.

Viwango vya riba vya Malawi vimeshuka chini kutoka kama asilimia 35 hadi kufikia asilimia 15 kwa hivi sasa na kwamba kiwango cha kupanda kwa gharama za maiasha kimeshuka kutoka asilimia 17.5 hadi kuwa asilimia 7.9 katika kipindi hicho hicho.

Waziri wa biashara na viwanda wa Malawi Henry Mussa amedokeza kwamba Malawi inapanga kufanya ziara zaidi za biashara mwaka huu ambapo nchi yake hivi sasa inazilenga Marekani,India na Japani.

Baraza la Jumuiya ya Madola linafanya kazi kwa ajili ya kutowa uongozi wa kuboresha uingizaji wa biashara ya kimataifa na uwekezaji na hiyo kuanzisha fursa mpya za biashara na kuemdeleza utawala bora na kuingiza uwajibikaji wa kijamii katika mashirika makubwa,inataka kupunguza pengo la digitali na kuziingiza nchi zinazoendelea katika soko la dunia.

Ziara ya Baraza la Biashara la Jumuiya ya Madola nchini Malawi CBC inafuatia Kikao cha Uwekezaji nchini Malawi kilichofanyika London mwezi wa April mwaka huu na kuvutia utashi mwingi katika uwekazaji nchini Malawi.