1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Leipzig na Bayern ziko juu Bundesliga

Sekione Kitojo
24 Oktoba 2016

Bayern Munich imeendelea kushikilia usukani wa ligi ya Ujerumani Bundesliga ikifuatiwa na timu iliyopanda daraja msimu huu RB Leipzig wakipishana kwa pointi mbili, wakati Hertha inafuatia ikiwa nafasi ya tatu.

https://p.dw.com/p/2Rdoe
Deutschland Bundesliga RB Leipzig gegen Werder Bremen
Vijana wa Leipzig wakifurahia baoPicha: Getty Images/Bongarts/M. Kern

Mabingwa  mara  nyingi  wa  Bundesliga  kutoka  mjini Munich , Bayern  Munich, katika  mchezo  wa  nane  wa ligi  ya  Ujerumani  wako  katika  nafasi  waliyoizowea  juu kileleni , lakini  mambo  hayako  kawaida  kwa  mazowea ya  ligi  hiyo  mara  hii. Nyuma  ya  mabingwa  hao  watetezi ziko  timu  za  RB Leipzig, Hertha  Berlin, Hoffenheim  na FC Kolon  katika  msafara  wa  kuifukuzilia  Bayern, na katika  nafasi  ya  sita  ndipo inapatikana  Borussia Dortmund  makamu  bingwa  msimu  uliopita. Vilabu vingine  vyenye uwezo  mkubwa  kama  Wolfsburg  na Schalke  vinatambaa  bado  kutoka  chini  ya  msimamo wa  ligi  katika  eneo la robo  ya  tatu  ya  ligi  hiyo.  RB Leipzig ilifanikiwa  kuchupa  hadi  nafasi  ya  pili  nyuma  ya Bayern  baada  ya  jana  Jumapili  kuicharaza  Werder Bremen kwa  mabao  3-1  ikiwa  nyumbani.

Fußball Bundesliga 8. Spieltag FC Bayern gegen Mönchengladbach
Wachezaji wa Bayern Munich wakishangiria bao baada ya Douglas Costa kupachika bao la pili dhidi ya GladbachPicha: Getty Images/Bongarts/A. Hassenstein

Kocha  wa  RB Leipzig Ralph Hasenhüttl  anasema  hata hivyo  haikuwa  rahisi  ushindi  dhidi  ya  Werder  Bremen.

"Mungu  ashukuriwe  tumeweza  kufanikiwa, kushinda mchezo  huu. Iwapo tulistahili , bila  shaka , kwa  jumla tulipata  nafasi  nyingi , kona  nyingi. Lakini  unaweza kuona  kwamba , Bremen  ni  timu  ambayo  ina ari  kubwa, timu  ambayo  haijifichi  na  ndio  sababu  ilikuwa  vigumu, na  ilibidi  tutumie uwezo  wetu  wote kuweza  kuhimili vishindo."

Deutschland VfL Wolfsburg - RB Leipzig
Kocha wa RB Leipzig Ralph HasenhuettlPicha: Getty Images/Bongarts/S. Franklin

Inafurahisha  kuona  kwamba  timu zilizoko  juu  zinatoka katika  kundi  la  timu zinazoitwa  za  "kiwango  cha  kati", alisema  hayo  meneja  wa  spoti  wa  Borussia Moenchengladbach  Max Eberl  baada  ya  kipigo  cha mabao  2-0 nyumbani  kwa  Bayern  Munich  siku  ya Jumamosi  jioni. Baada  ya  kung'ara  katika  Champions League  katikati  ya  wiki  dhidi  ya  Celtic  Glasgow  kwa kuichapa  mabao  2-0 , Borussia  Moenchengladbach haikuweza kufurukuta  na  pia  nguvu  ziliwaishia. Amekiri Eberl  kwamba  kikosi  chake  hakikuwa  na  uwezo  wa kupambana   katika  Champions League  na  baada  ya siku  tatu  kupambana  katika  ligi.

Inaelekea  ukweli  huo  umedhihirika  kwa  Bayer Leverkusen pia ambayo  ilikubali  kipigo  cha  mabao 3 bila majibu  dhidi  ya  Hoffenheim  ambapo  mshambuliaji  wa Leverkusen  aliyetokea  Hoffenheim  msimu  uliopita  Kevin Volland  alitolewa  nje  kwa  kadi  nyekundu  dakika  tano tangu  mchezo  kuanza  na  kuiacha  timu  yake  hiyo mpya  ikiwa  pungufu uwanjani  kwa  dakika  takriban 85.  Kevin Volland  alisema.

Deutschland Bayer Leverkusen - 1899 Hoffenheim Schiedsrichter Bastian Dankert
Kevin Volland karibu na mwamuzi aliyenyanyua mikono juu. Alitolewa nje baada ya kumwangusha mchezaji wa Hoffenheim .Picha: picture alliance/dpa/Revierfoto

"Nafikiri  hii  ilikuwa  hali  mbaya  sana  kwangu  mimi. Hakuna  mtu  anayetamani  kitu  kama  hicho, na  pia  hata timu,  kupambana  huku mkiwa   pungufu  kwa  mtu mmoja . Kwa  hilo  hata  mimi  nashindwa  kusema  lolote, ni  machungu  matupu."

Hertha  Berlin  inashikilia  nafasi  ya  tatu  katika  msimamo wa  ligi  ikiwa  na  pointi 17  tatu  nyuma  ya  Bayern Munich baada  ya  kuishinda  FC Kolon  kwa mabao 2-1  siku  ya Jumamosi na  kuizawadia  Kolon  kipigo  chake  cha kwanza  msimu  huu. Mlinzi  wa  pembeni  wa  Hertha Berlin  aliyesababisha  bao  la  kwanza  chipukizi Mitchell Weiser  anasema.

"Nafikiri  baada  ya  mapumziko , hadi  dakika  ya  16 tulikuwa  tumelegea  kidogo  na  Kolon  walituadhibu pia. Lakini  kile  ninachokiona  kuwa  kizuri  kutoka  kwetu, baada ya  hapo  tulifunga  mlango  wetu na  kutoa  jibu. Na huu  ndio  uzuri  wetu  na  ubora  wa  timu yetu."

Borussia  Dortmund  nusura  ionje  kipigo  siku  ya Jumamosi  wakati  hadi  kipindi  cha  kwanza  kinamalizika wapinzani  wao  Ingolstadt  ilikuwa  ikiongoza  kwa  mabao 2-0. Kipindi  cha  pili  kilishuhudia  mabao manne wakati Borussia  Dortmund  ikijikakamua  baada  ya  mchezo  wa Chapions League  dhidi  ya  Sporting Lisbon   na kurejesha  mabao  matatu  dakika  moja  kabla  mchezo kumalizika na  kuokoa  pointi  moja  muhimu  inayowaweka katika  nafasi  ya  sita.

Fußball Bundesliga FC Ingolstadt v Borussia Dortmund Ausgleich Pulisic
Christian Pulisic wa Borussia Dortmund (mbele) akishangiria bao la kusawazisha dhidi ya Ingolstadt pamoja na wachezaji wenzakePicha: Imago/Eibner

Wolfsburg ndio  iliyoathirika  zaidi wiki  hii. Baada  ya  kutengana  na  kocha  wake  Dirter Hecking  na  kumteau  kocha  wa  kikosi  cha  pili  cha  timu hiyo Valerien Ismail  kuchukua  hatamu  za  kukiongoza kikosi  hicho  hali  haikuwa  shwari. Kwani  walibamizwa mabao 3-1  na  Darmstadt. Huyu  hapa  kocha  Valerien Ismail.

"Tulitaka  kupata  pointi  leo. Tulitaka  kujaribu , kila  kitu tulichonacho. Lakini  haikuwezekana. Kutokana  na matokeo  tumesikitishwa. Lakini  nadhani, timu  ilikuwa  ina ari, ilijitayarisha  vizuri. Ilijionesha  hivyo, lakini  baada  ya siku  tatu  sidhani  kama  kuna  mtu  ambaye  anaweza kuwa  na  matumaini  makubwa. Na  pia  iwapo mchezaji anapewa  kadi  nyekundu  baada  ya  dakika  25, ni  dhahiri kwamba  inakuwa  vigumu  sana, sana."

Fußball Bundesliga 8. Spieltag, SV Darmstadt 98 - VfL Wolfsburg
Kocha wa mpito wa VFL Wolfsburg Valerien IsmailPicha: Reuters/K. Pfaffenbach

Hata  hivyo  kesho  Jumanne  na  Jumatano  viwanja kadhaa  nyasi  zitawaka  moto  wakati  kutakapokuwa  na kinyang'anyiro  cha  kombe  la  Ujerumani  DFB Pokal duru ya  pili.  Mabingwa  Bayern  Munich  watajitupa  uwanjani siku  ya  Jumatano  kupambana  na   majirani  zao Augsburg, wakati  makamu  bingwa  wa  DFB Pokal  Borussia  Dortmund inapambana  na  Union Berlin. Siku  hiyo  hiyo  Schalke itakuwa  uwanjani  kupambana  na  Nurmberg  wakati  FC Kolon  inaikaribisha  Hoffenheim. Kesho  Jumanne  Lotte inaikaribisha  Bayer Leverkusen , wakati  St. Pauli inakabiliana  na  Hertha Berlin  na  Borussia  Moenchengladbach  itapimana nguvu  na  VFB Stuttgart  nayo  Halle  inaikaribisha  Hamburg SV.

Premier League

Kipigo  cha  mabao  4-0  dhidi  ya  Chelsea  kimemletea fadhaa  kocha  wa  Manchester  United  Jose Mourinho wakati  akirejea  katika  klabu  yake  hiyo  ya  zamani  ya darajani  jana  Jumapili.

Mourinho  alionekana  akiwa  na  uso  wa  huzuni   jioni  ya jana  wakati  kocha  wa  Chelsea  Antonio Conte alionekana  kufurahia  sana  kile  alichokiona  uwanjani. Mtaliani  huyo  aliwahamasisha  mashabiki  kushangiria zaidi   ili  kupata  mabao  mengine  baada  ya  bao  la  nne la  N'golo Kante kitu  ambacho  Mourinho  hakufurahishwa nacho. Ripoti za  vyombo  vya  habari  vya  Italia  zimesema Mourinho  alimwambia  Conte  mwishoni  mwa  mchezo huo, "hupaswi  kushangiria  kama  ulivyofanya  wakati ukiwa  na  mabao 4-0. Unaweza  kufanya  hivyo  baada  ya bao 1-0, vinginevyo  inadhalilisha kwa  upande  wetu."

Fußball UEFA Europa League Feyenoord Rotterdam - Manchester United
Kocha Jose Mourinho wa Manchester UnitedPicha: Getty Images/D. Mouhtaropoulos

Conte  alikana  kufanya  kosa  lolote. Mourinho  hata  hivyo hakueleza  nini  alichosema  katika  mahojiano  baada  ya mchezo  huo na  kusema  tu , maneno  aliyomwambia Conte  yalikuwa  ni  kwa  yeye  binafsi na  sio  kwa  mtu mwingine.

Manchester  City  bado  inaongoza  ligi  hiyo  lakini  kwa wingi  wa  mabao , ikifuatiwa  na  Arsenal  London  na Liverpool , baada  ya  Machester  City  kutoka  sare  ya  bao 1-1  na  Southamptom siku  ya  Jumamosi.

Hata  hivyo  timu  hizo Manchester  United  na  Manchester City  zitarejea  tena  uwanjani  siku  ya  Jumatano  katika pambano  la  kombe  la  ligi  duru  ya  nne. Kesho Jumanne Arsenal  itaikaribisha  Reading, Bristol itapambana  na  Hull City, wakati Liverpool  ni  wenyeji  wa Tottenham Hotspurs. Chelsea  itapambana  na  West Ham siku  ya  Jumatano  na  Southampton ina  miadi  na Sunderland.

Pep Guardiola UEFA Champions League
Kocha wa Manchester City Pep GuardiolaPicha: picture-alliance/dpa/P. Powell

Ballon d'Or

Mchezaji  bora  wa  mwaka  mara  tatu duniani  Cristiano Ronaldo  atapambana  na  mchezaji  mwenzake  katika Real  Madrid Gareth Bale  kuwania  tuzo  hiyo  ya  Ballon d'Or, mpira  wa  dhahabu  mwaka  huu. Wadhamini  wa tuzo  hiyo , jarida  la  michezo  la  Ufaransa  linatoa  majina ya  wachezaji 30 kwa  awamu  ya wachezaji  watano watano  leo  Jumatatu.

CAF Champions League

Katika  bara  la  Afrika ,  bingwa  wa  bara  hilo  kwa  vilabu alipatikana  jana  Jumapili, ambapo  Mamelodi  Sundowns ya  Afrika  kusini  ilitawazwa  kwa  mara  ya  kwanza  rasmi kuwa  mabingwa  wa  CAF  Champions  League  licha  ya kubwagwa  kwa  bao  1-0  na  Zamalek  ya  Misri  mjini Alexandria  jana. Stanley Ohawuchi  raia  wa  Nigeria  ndie aliyeipatia  Zamalek  bao  hilo  katika  dakika  ya  64, lakini halikutosha  kuiokoa  timu  hiyo  wenyeji  kwa  kuwa Mamelodi  ilikuwa  tayari  imepata  mabao 3-0  nyumani wiki  moja  iliyopita  katika  mchezo  wa  kwanza  uliofanyika mjini  Pretoria .

Omar Mahmoud Zamalek Ägypten Fussball
Omar Mahmoud wa Zamalek ya Misri. Timu iliyocheza na Mamelodi Sundowns wa Afrika kusini katika fainali ya kombe la Champions League barani AfrikaPicha: AFP/GettyImages

Ni ushindi  wa  kujivunia  kwasababu  wababe  hao  wa Afrika  kusini  waliondolewa  katika  duru  za  mwisho  za mchujo mwezi  Aprili  mwaka  huu  na  kurejeshwa  tena katika  kinyang'anyiro  hicho  wakati  wapinzani  wao kutoka  Jamhuri  ya  Kidemokrasi  ya  Congo  kuondolewa. Ubingwa  huo umewapa  Sundowns kitita  cha  euro  milioni 1 na  lakini  tatu  na  kupata  fursa  ya  kuliwakilisha  bara la  Afrika  katika  michuano  ya  kombe  la  dunia  la  vilabu la  FIFA nchini  Japan  mwezi  Desemba.

Mbio za  magari

USA Austin Formel 1 Sieger Hamilton mit Pokal
Bingwa wa dunia wa mbio za magari Lewis Hamilton wa UingerezaPicha: picture-alliance/AP Photo/E. Gay

Kwa upande  wa  mbio  za  magari ,  bingwa  mtetezi  Lewis Hamilton atawajibika  kukaza  uzi  baada  ya  kurejesha uhai  katika  matumaini  ya  ubingwa  wa  Formula  one, jana  na  analazimika  kushinda  katika  mbio  za  Grand prix  za  Mexico  iwapo  anataka  kunyakua  tena  ubingwa huo. Bingwa  huyo alishinda  mbio  za Texas Grand prix nchini  Marekani  jana  lakini  Nico Rosberg  anayeendesha pia  gari  ya  Meecedes  anaendelea  kushikilia  uongozi wa  pointi  26, wakati  mbio  tatu  zimebakia  msimu  huu.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo  / afpe / dpae / rtre

Mhariri: Iddi Ssessanga