1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

COVID-19: Mataifa 47 yakabiliwa na hali ngumu zaidi

3 Desemba 2020

Umoja wa Mataifa unasema nchi ambazo hazijaendelea kiviwanda duniani mwaka huu wa 2020 zinapitia kipindi kigumu zaidi cha kiuchumi kuwahi kushuhudiwa katika kipindi cha miaka thelathini iliyopita.

https://p.dw.com/p/3mBDh
Deutschland | Coronakrise: Krankenhaus in Leipzig
Picha: picture alliance/dpa/dpa-Zentralbild

Hayo ni katika ripoti ya shirika la Shirika la Umoja wa Mataifa la Biashara na Maendeleo - UNCTAD. 

Katika ripoti yake ya mwaka 2020 ya nchi ambazo hazijaendelea kiviwanda, Shirika la Umoja wa Mataifa la Biashara na Maendeleo UNCTAD limebashiri kuwa kupungua kwa viwango vya mishahara, ukosefu mkubwa wa ajira na kuongezeka kwa mapungufu ya fedha katika bajeti za nchi hizo, mambo yaliyosababishwa na janga la virusi vya corona, huenda yakasababisha watu milioni 32 kutumbukia katika uchochole katika nchi hizo zilizoorodheshwa kama zilizo kwenye kiwango cha chini cha maendeleo.

Wakati madhara ya kiafya yaliyosababishwa na virusi vya corona katika nchi hizo yakiwa si makubwa kama ilivyofikiriwa na wengi, ripoti hiyo inasema madhara ya kiuchumi ni makubwa mno.

Makadirio ya ukuaji wa uchumi katika nchi hizi yalipitiwa upya kutoka asilimia 5 na sasa unatarajiwa kuwa asilimia 0.4 kati ya Oktoba mwaka 2019 na Oktoba 2020 jambo litakalopelekea kupungua kwa kiwango cha mapato ya nchi hizo kwa asilimia 2.6 katika Mwaka 2020.

Äthiopien Industriegebiet in Hawassa
Kupungua kwa mahitaji ya bidhaa kumesababisha pia kuongezeka kwa ugumu kwenye mataifa hayo kiuchumi.Picha: Imago/Xinhua Afrika

Kushuka pakubwa kwa uhitaji wa bidhaa zinazotoka katika nchi maskini duniani ni jambo ambalo limesababisha kushuka kwa bei za baadhi ya bidhaa muhimu zilizokuwa zinategemewa na nchi hizo. Nchi ambazo uchumi wake unategemea sana kuuza bidhaa kama madini na vyuma au nguo, zimeathirika pakubwa kwa sababu bei za bidhaa zao katika masoko ya nje zilishuka ghafla na kiwango cha bidhaa hizo kununuliwa pia kikapungua kwa kiasi kikubwa.

Katibu Mkuu wa shirika hilo la Umoja wa Mataifa Mukhisa Kituyi katika taarifa iliyotolewa pamoja na ripoti hiyo amesema viwango vya maisha vya nchi hizo ambavyo tayari viko chini, vinaendelea kushuka zaidi na viwango vya umaskini vinaendelea kuongezeka na kuzirejesha nyuma nchi hizo katika maendeleo madogo zilizokuwa zimeyapata kabla janga la virusi vya corona.

Wataalam wanaamini kwamba uzoefu wa awali wa kukabiliana na majanga pamoja na masuala ya idadi ya watu katika nchi hizo ni mambo yaliyozisaidia nchi hizo kukabiliana vyema na janga la virusi vya corona katika miezi yake ya kwanza.

Lakini UNCTAD linaonya kuwa kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya corona katika nchi hizo huenda kukasababisha kulemewa kwa mifumo ya afya ambayo tayari haijaimarika.

Ripoti hiyo inasema kuimarika tena kwauchumiwa nchi hizo itakuwa ni kibarua kikubwa iwapo uwezo wao wa uzalishaji hautaimarishwa.

Katibu Mkuu wa shirika hilo la Umoja wa Mataifa Mukhisa Kituyi ametoa wito kwa jamii ya kimataifa kuzisaidia nchi hizi kwa kuweka mpango unaolenga kuimarisha uwezo wao wa uzalishaji.