Champions League kuanza tena kutimua vumbi
25 Novemba 2019Jose Mourinho alikuwa na mwanzo mzuri katika maskani yake mapya ya Tottenham baada ya kupata ushindi katika mechi yake ya kwanza kwenye Premier League
Na anataraji kuendeleza mwanzo huo mzuri wakati Spurs watawaalika Olimpiakos kesho Jumanne katika Champions League. Ushindi utawahakikishia tiketi ya hatua ya mtoano pamoja na Bayern Munich kutoka Kundi B huku kukiwa na mechi moja ya ziada.
Timu tatu tayari zimefuzu baada ya mechi nne kati ya sita za hatua ya makundi. Nazo ni Bayern, Paris Saint-Germain na Juventus.
Atletico Madrid wanalenga kufuzu pamoja na Juventus kutoka Kundi D lakini wanafahamu kuwa mechi yao ya kesho haitakuwa rahisi maana Cristiano Ronaldo anatarajiwa kurejea baada ya kupumzishwa katika mechi ya ligi.
Kocha wa Borussia Dortmund Lucien Favre hana kabisa nafasi ya kufanya kosa wakati timu yake itashuka dimbani na Barcelona Jumatano. Ushindi utaipa BVB, ambayo iko pointi moja nyuma ya Barca katika Kundi F, tiketi ya hatua ya mchujo.
Real Madrid wanaweza kufuzu katika Kundi A na labda kulipiza kisasi dhidi ya PSG hapo kesho. PSG waliwazidi nguvu Madrid kwa kuwabamiza 3-0 mjini Paris mwezi Septemba.
Kinara wa Kundi C Manchester City atafuzu kama ataibwaga Shakhtar Donetsk nyumbani kesho. Liverpool iko mbele ya Napoli kwa pointi moja kabla ya kukutana Jumatano katika Kundi E, huku Salzburg ikipiga dhidi ya Genk.
Katika Kundi H, Ajax, Chelsea na Valencia wote wana pointi saba. Valencia inaialika Chelsea Jumatano wakati Ajax ikicheza ugenini dhidi ya Lille. Katika Kundi G, Leipzig na Lyon zinaweza kufuzu kwa kuzichapa Benfica na Zenit St. Petersburg Jumatano.