1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiUfaransa

Seneti Ufaransa yaidhinisha mageuzi ya mfumo wa pensheni

12 Machi 2023

Bunge la Seneti la Ufaransa lilipiga kura jana Jumamosi na kuidhinisha mageuzi ya mfumo wa pensheni uliokosolewa pakubwa nchini humo, saa chache tu baada ya waandamanaji kumiminika barabarani kuipinga sera hiyo.

https://p.dw.com/p/4OZ1G
Frankreich | Protest Rentenreform
Picha: Sarah Meyssonnier/REUTERS

Maseneta waliidhinisha mageuzi ya mfumo huo wa pensheni kwa kupiga kura 195 za ndio dhidi ya 112 za hapana, kumaanisha zimesalia hatua chache tu kabla ya mageuzi hayo kutangazwa kuwa sheria.

Kamati maalum sasa ina jukumu la kuandaa rasimu ya mwisho, ambayo itawasilishwa katika bunge la seneti la lile la kitaifa kwa ajili ya kura ya mwisho.

Waziri Mkuu Elisabeth Borne ameliambia shirika la habari la AFP baada ya kura hiyo kwamba, hatua muhimu imechukuliwa na bunge la Seneti juu ya mageuzi ya mfumo wa pensheni huku akiamini kuwa, wana idadi kubwa ya wabunge ambao wataipitisha na kuwa sheria.

Vyama vya wafanyakazi ambavyo vimepinga vikali mageuzi ya mfumo wa pensheni, bado vilikuwa na matumaini jana kwamba Macron angerudi nyuma, ingawa maandamano ya jana yalikuwa madogo sana tofauti na siku za nyuma.