1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern, Leipzig, Dortmund zarejea kwa ushindi, Schalke hoi

4 Januari 2021

Baada ya mapumziko mafupi ya wiki mbili, kivumbi kilianza tena kutimuliwa mwishoni mwa wiki huku kukiwa na ushindi kwa Bayern, Dortmund na Leipzig katika upande wa juu wa ligi. Hali bado ni tete kwa washika mkia Schalke

https://p.dw.com/p/3nVB3
Fußball Bundesliga Bayern München - Mainz 05
Picha: Andreas Gebert/AFP/Getty Images

Taswira ya kinyang'anyiro cha ligi msimu huu mpaka sasa ni ile ile kwamba Bayern Munich wanaongoza msimamo wa ligi wakati mzunguko wa pili wa msimu ukianza. Lakini tofauti na misimu iliyopita ambapo wangekuwa tayari mabingwa watarajiwa kwa wakati kama huu, mambo ni magumu msimu huu kwa sababu wanaongoza kwa pengo la pointi mbili tu kileleni. Ushindi wao wa 5 – 2 dhidi ya Mainz unaonekana kuwa mzuri lakini ilikuwa mechi ya nane mfululizo kwa Bayern kulazimika kutoka nyuma na kunyakua pointi tatu. Hii ina maana mwanzo mbaya kama huo katika mechi unaweza kuwadhuru dhidi ya mpinzani aliye bora.

Unapocheza namna ile katika kipindi cha kwanza kama Bayern Munich basi hata sisi wachezaji pia tunajiuliza maswali kambini. Na tunafahamu hatupaswi kumaliza mechi kwa njia ile na kuwa tunapaswa kuimarisha mchezo. Kwa kuanza na mtazamo.

Bundesliga - Borussia Dortmund v VfL Wolfsburg
Dortmund ilimkaribisha nyota Haaland kutokea mkekaniPicha: Leon Kuegeler/POOL/AFP/Getty Images

Ushindi wa Bayern umewapa pointi 33 kwenye mechi 14. RB Leipzig wana 31 baada ya ushindi wao wa 1 – 0 dhidi ya VfB Stuttgart.

Timu nyingine inayoonekana kutoa ushindani kwa Bayern msimu huu ni Bayer Leverkusen lakini kocha wake Peter Bosz ameinua kitambaa cheupe katika kinyang'anyiro cha ubingwa, baada ya kichapo cha pili mfululizo jana kushamwishi kuwa Bayern kwa mara nyingine tena watakuwa mabingwa, kwa mwaka wao wa tisa mfululizo.

Leverkusen ilifungwa tena 2 – 1 dhidi ya Eintracht Frankfurt na sasa ipo nafasi ya tatu na pengo la pointi tano

Tunafahamu kuwa timu yetu, timu yangu, inaweza kuimarika zaidi. Nadhani tumeonyesha hilo katika kila mchezo. Na leo hakukuwa na kitu kama hicho. tulistahili kupoteza.

Borussia Dortmund wamepenyeza tena katika nafasi ya nne za kwanza baada ya ushindi wa 2 – 0 dhidi ya nambari sita Wolfsburg. Manuel Akanji ni mmoja wa waliofunga mabao ya BVB

Pointi tatu bila shaka ndio kitu muhimu. Ulikuwa ni mwanzo mzuri kwa mwaka mpya. Tuna mechi nyingine muhimu wiki ijayo. hakika, tuna mechi muhimu pekee. Tunafurahia ushindi wa leo na kisha kesho tunaendelea kujiandaa kwa mchezo unaofuata. Na tunataka kuchukua pointi tatu tena.

Fußball Bundesliga Hertha BSC - Schalke
Schalke hawajashinda katika mechi 30 mfululizoPicha: Tim Rehbein/RHR-FOTO/imago images

Katika upande wa mkia, Schalke wamebaki na mechi moja wakifikia rekodi ya Bundesliga ya mechi 31 mfululizo bila ushindi. Kocha mpya Christian Gross alishindwa kupata ushindi katika mechi yake ya kwanza tangu alipochukua usukani. Kipigo cha 3 – 0 mikononi mwa Hertha Berlin kinamaana wamecheza mechi 30 mfululizo bila ushindi.

Mpinzani wao ajaye ni TSG Hoffenheim, Jumamosi ijayo na kocha Gross ameonekana mwenye matumaini makubwa ya kuyabadilisha mambo katika timu ambayo mshambuliaji wake Mark Uth amesema haiwezi kutoa ushindani wowote

Tukicheza kama tulivyocheza katika kipindi cha pili, hakika hatuwezi kwenda popote. Kipindi cha kwanza kiliwa sawa lakini hatuwezi kusema dakika 30 za kwanza zilikuwa nzuri. Mchezo wa kandanda ni dakika 90 na kama unafungwa kwa urahisi, labda naweza kukubali lawama kufungwa 1 - 0 katika kipindi cha kwanza. Tunafungwa kwa urahisi sana.

Gross ni kocha wa nne kuchukua usukani msimu huu baada ya David Wagner, Manuel Baum na kaimu kocha aliyesimamia mechi mbili Huub Stevens.

afp, ap, dpa