Baada ya vita Iran, biashara ya dunia itastawije haraka?
31 Machi 2026
Wakati wale wenye matumaini wakianza kuhisi kwamba vita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran vilikuwa karibu kumalizika, mgogoro huo wa mwezi mzima unachukua mwelekeo mwingine tena.
Wakati mmoja, Rais wa Marekani Donald Trump anaionya Tehran kwamba hakutakuwa na "kurudi nyuma” kuhusu mashambulizi yaliyoongezwa ya Marekani, na mara inayofuata anaahirisha vitisho hivyo vya kulenga miundombinu ya nishati ya Iran kwa mara ya pili.
Iran, kwa upande wake, inaruhusu idadi ndogo ya meli kupita katika Mlango wa Hormuz, huku ikikanusha kuwa mazungumzo yoyote ya kusitisha vita yanaendelea.
Wataalamu wengi wanakubaliana juu ya jambo moja muhimu: kadiri mzozo huu unavyoendelea kwa muda mrefu, ndivyo athari zake zitakavyokuwa mbaya zaidi kwa usambazaji wa nishati duniani, mfumuko wa bei na uthabiti wa uchumi. Kila wiki ya ziada ya usumbufu inaongeza gharama kwa watumiaji na biashara huku ukuaji ukipungua.
Benki ya Hifadhi ya Shirikisho ya Dallas, ambayo ni sehemu ya mfumo wa benki kuu ya Marekani, ilitabiri mapema mwezi huu kwamba kufungwa kwa mlango huo kwa miezi mitatu au zaidi kungesababisha ukuaji wa Pato la Taifa la dunia kupungua kwa asilimia 2.9 kwa mwaka katika robo ya pili ya mwaka.
Wakati wowote Hormuz — njia nyembamba inayopitisha asilimia 20 ya biashara ya mafuta duniani — itakapofunguliwa tena, kasi ambayo uzalishaji wa mafuta na gesi pamoja na usafiri wa meli za mafuta utaanza tena itaamua jinsi uchumi wa dunia utakavyoweza kufufuka haraka.
Kulinda Mlango wa Hormuz
Kampuni za usafirishaji haziwezi kuanza tena kupita katika njia hii ya kimkakati hadi ada za bima zipungue kwa kiasi kikubwa na operesheni ya kuaminika ya ulinzi wa majini wa kimataifa iwe imewekwa. Hii inaweza kujumuisha meli za kivita za Jeshi la Wanamaji la Marekani, doria za angani na vyombo vya kuondoa mabomu ya baharini.
Mataifa washirika wa NATO wa Ulaya, yakiwemo Ujerumani, Ufaransa na Uingereza, yameonyesha utayari wa kujiunga na doria hizo mara mapigano yatakapokoma. Japan, Australia, Korea Kusini, Canada, Umoja wa Falme za Kiarabu na Bahrain pia zinatarajiwa kushiriki.
Kuondoa mabomu ya baharini katika mlango huo pekee kunaweza kuchukua takribani wiki mbili, kulingana na ripoti ya Bloomberg iliyomnukuu Jennifer Parker, profesa msaidizi katika Taasisi ya Ulinzi na Usalama ya Chuo Kikuu cha Western Australia.
Mara tu Hormuz itakapochukuliwa kuwa salama kwa urambazaji, msongamano wa takribani meli 1,900 zilizokwama — nusu yake zikiwa zinabeba mafuta, LNG au kemikali nyingine — unaweza kusafishwa ndani ya siku chache hadi wiki chache, mradi upungufu wa wafanyakazi wa meli utatatuliwa.
"Kwa wakati huu, kimsingi ni mashindano ya kufika sokoni,” alisema Aditya Saraswat, mkurugenzi wa utafiti wa kanda za Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini katika kampuni ya uchambuzi ya Rystad Energy yenye makao yake Norway, akizungumza na DW. Aliongeza kuwa kusafisha msongamano wa Hormuz kungewapa wazalishaji wa Ghuba "akiba ya mwezi mmoja” kuongeza uzalishaji.
Hata hivyo, changamoto za vifaa zitaendelea. Kabla ya vita, takribani meli 130 hadi 140 zilipita Hormuz kila siku, lakini mtiririko huo huenda ukawa polepole zaidi kwa muda mrefu kadiri doria za kijeshi zitakavyohitajika.
Kuanzishwa upya kwa uzalishaji wa mafuta na gesi
Mbali na kufunguliwa tena kwa Hormuz, wazalishaji wa Ghuba watahitaji uhakika kwamba hali ya usalama imetulia katika vituo vyao vya mafuta na gesi. Hata kwa makubaliano ya amani ya haraka, wachambuzi wanasema kuanzisha tena uzalishaji katika maeneo mengi kunaweza kuchukua wiki kadhaa.
"Mtambo wa mafuta uliopunguzwa uzalishaji huchukua wastani wa wiki mbili hadi tatu kurejea kawaida,” alisema Saraswat. "Kwa kufungwa kabisa, unazungumzia takribani mwezi mmoja na nusu.”
Aliongeza kuwa kadiri vituo vya mafuta na gesi vinavyokaa bila kufanya kazi kwa muda mrefu, ndivyo ukaguzi wa matengenezo unavyohitajika kuwa wa kina zaidi kabla ya kuanza tena.
Kuongeza uzalishaji wa mafuta na gesi ni kama kuhuisha gari la zamani baada ya kuegeshwa kwa miezi kadhaa. Lazima uchunguze kwa makini na kurekebisha mabomba, visima, pampu, mitambo ya usindikaji na visafishaji kwa ajili ya kutu, vizuizi, uharibifu wa maji na masuala ya usalama.
Kulingana na Shirika la Kimataifa la Nishati (IEA), angalau maeneo 40 muhimu ya nishati ya Ghuba yameharibiwa "kwa kiwango kikubwa au kikubwa sana” na mashambulizi ya Iran. Wachambuzi wa nishati wameonya kuwa baadhi ya miundombinu, hasa mitambo ya LNG, inaweza kuhitaji miaka kadhaa kurekebishwa.
Qatar imesema kuwa kituo chake cha LNG cha Ras Laffan, ambacho ni kikubwa zaidi duniani kwa uzalishaji na usafirishaji wa LNG, kinaweza kuhitaji hadi miaka mitano kurejesha shughuli kikamilifu.
Kabla ya mashambulizi ya makombora ya Iran kusababisha uharibifu mkubwa, Qatar ilikuwa ikisambaza takribani humusi moja ya LNG duniani. Sasa takribani asilimia 17 ya uwezo wa mauzo ya LNG wa taifa hilo haitakuwepo sokoni kwa muda mrefu.
Mara tu mafuta na gesi vitakapoanza tena kusafirishwa, wazalishaji wataongeza uzalishaji hatua kwa hatua na kurekebisha matatizo yaliyobaki katika visafishaji na mabomba. Hii inaweza kuchukua wiki chache zaidi hadi miezi kadhaa, kulingana na wachambuzi wa sekta ya mafuta.
Kuanzisha tena uzalishaji wa mbolea na njia za makontena
Viwanda vya mbolea vitahitaji ukaguzi sawa wa usalama kabla ya kuanza tena uzalishaji ili kusaidia kulinda usalama wa chakula duniani, ambao tayari unatishiwa na kupanda kwa bei, hali inayowalazimu wakulima kupunguza matumizi ya virutubisho muhimu vya udongo.
Kanda ya Ghuba ni msambazaji muhimu wa mbolea za nitrojeni, ikichangia takribani asilimia 40 ya urea inayosafirishwa kwa njia ya bahari duniani na robo ya mauzo ya amonia. Nchi za Ghuba ya Kiarabu pia ni wazalishaji wakubwa wa viambato viwili vinavyotumika katika uzalishaji wa fosfati.
Kulingana na Josh Linville, makamu wa rais wa mbolea katika kampuni ya huduma za kifedha ya Marekani StoneX, fosfati inaweza kuwa na changamoto zaidi kuliko mbolea za nitrojeni kutokana na gharama za uzalishaji ambazo tayari ni kubwa.
"Hata kama tutaanza kuona upatikanaji ukiboreka ... sidhani kama tunaweza kuhimili kushuka zaidi kwa bei kabla [wazalishaji wa fosfati] hawajafunga uzalishaji. Hawatazalisha kwa hasara,” alisema Linville kwenye chaneli ya YouTube ya kampuni hiyo.
Usafirishaji wa makontena, ambao hubeba bidhaa zinazozalishwa katika eneo la Ghuba na kutoka Asia kwenda Ulaya, pia umeathirika vibaya na kufungwa kwa Hormuz, huku meli kadhaa zikiwa zimekwama. Meli zinazoingia katika bandari kubwa ya Jebel Ali huko Dubai, kitovu kikubwa zaidi cha usafirishaji wa kati Mashariki ya Kati, imepungua tangu Februari 28, kulingana na mwendeshaji, kampuni ya DP World.
Meli za makontena zinazoelekea Ulaya zinakabiliwa pia na changamoto ya Mlango wa Bab el-Mandeb, ulioko kusini mwa Bahari ya Shamu. Ingawa mlango huo uko wazi, kampuni nyingi kubwa za usafirishaji zinauepuka kutokana na vitisho vipya kutoka kwa waasi wa Houthi wanaoungwa mkono na Iran. Waasi hao walioko Yemen walifanya mashambulizi dhidi ya meli mwaka 2023–24 zinazohusishwa na vita vya Israel huko Gaza.
Kampuni nyingi zimebadilisha njia kupitia Rasi ya Tumaini Jema kusini mwa Afrika, jambo linaloongeza muda na gharama za safari.
Taasisi ya Kiel ya Uchumi wa Dunia ya Ujerumani ilikadiria kuwa mataifa ya Ghuba, ikiwa ni pamoja na Iran, yana sehemu kubwa zaidi ya mauzo ya bidhaa 50 muhimu zisizo za madini duniani, ikiwa ni pamoja na chuma, almasi zisizokatwa, dhahabu ya unga na aloi za alumini. Mauzo haya yana thamani ya dola bilioni 773 kwa mwaka.
Athari zinazoendelea kwa mfumuko wa bei na minyororo ya usambazaji
Hata Hormuz itakapofunguliwa tena na uzalishaji wa Ghuba kuanza kuongezeka, athari za kiuchumi duniani hazitatoweka mara moja.
Watumiaji tayari wamehisi athari za kupanda kwa bei ya mafuta, huku upungufu wa petroli na dizeli ukianza kujitokeza Australia, Asia na Afrika. Minyororo mingine muhimu ya usambazaji, kuanzia mbolea hadi bidhaa za matumizi, inatarajiwa kukumbwa na upungufu wake katika wiki chache zijazo.
"Misukosuko ya bei imejitokeza mara moja; misukosuko ya vifaa itakuwa muhimu zaidi ndani ya miezi 2 hadi 3 ijayo,” alisema Peter Klimek, mkurugenzi wa Taasisi ya Uchunguzi wa Minyororo ya Usambazaji Austria, akizungumza na DW.
Ikiwa uzalishaji wa viwandani duniani utalazimika kupunguza uzalishaji kutokana na vita, Klimek alionya kuhusu "hali ya mfumuko wa bei pamoja na kudorora kwa uchumi,” inayojumuisha bei za juu, ukosefu wa ajira unaoongezeka na ukuaji dhaifu wa uchumi, hali ambayo alisema inaweza "kuchukua muda mrefu zaidi kutatuliwa.”