1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Atalanta Bergamo yaiduwaza Leverkusen kombe la Europa

23 Mei 2024

Rekodi ya msimu wa kutoshindwa ya Bayer Leverkusen imekatisha katika mechi ya 52 ya kampeni yao, baada ya kushindwa kufurukuta mbele ya Klabu ya Atalanta ya nchini Italia katika fainali ya Ligi ya Europa.

https://p.dw.com/p/4gAUW
Atalanta Bergamo - Bayer Leverkusen
Atalanta Bergamo imeiduwaza Bayer Leverkusen fainali ya Ligi ya UropaPicha: Federico Gambarini/AP/dpa/picture alliance

Zilikuwa zimesalia siku tano kufikia mwaka mzima tanguBayer Leverkusen na kocha wake chipukizi Xabi Alonso kupoteza mchezo wa soka.

Uhalisia wa michezo uliidhihirikia wazi timu yao Jumatano wakati mbio za bila kushindwa za bingwa mpya wa Ujerumani ziliposimama katika mchezo wake wa 52 wa msimu huu, fainali ya Ligi ya Europa.

Vijana wa Xabi Alonso wameduwazwa na wapinzani wao wanaonolewa na Kocha Gian Kuigi waliowatandika mabao 3-0, yote yakifungwa na Mnigeria Ademola Lookman, katika mechi ya fainali iliyochezwa mjini Dublin.

Kipigo cha Leverkusen cha 3-0 dhidi ya Atalanta na hat trick ya kushangaza ya Ademola Lookman kilikuwa kikubwa sana kiasi kwamba hakikuacha nafasi ya shaka.

UEFA Europa League - Ademola Lookman
Ademola Lookman ndiyo aligeuka mwiba mchungu kwa LeverkusenPicha: Hannah Mckay/REUTERS

"Kawaida sio kushindwa katika mchezo wa 52," Alonso alisema, akitafakari kipigo cha kwanza kwanza katika msimu wake wa kwanza kamili kama kocha wa timu ya daraja la juu. "Inapotokea katika mchezo mkubwa kama huu, inaumiza kwa hakika. Vipigo hivi kwenye fainali, hautavisahau."

Soma pia: Bayer Leverkusen kuandika historia itakapokutana na Atalanta?

Sasa Alonso lazima aiinue timu yake kwa ajili ya mechi nyingine ya fainali, ya 53 na ya mwisho ya msimu wa Leverkusen, akiwania taji la kombe la Ujerumani Jumamosi dhidi ya Kaiserslautern ya daraja la pili.

Lookman aandika jina lake katika vita vya historia

Lookman, ambaye alipambana kujiimarisha katika Ligi Kuu ya Uingereza akiwa na klabu za Everton, Fulham na Leicester City kabla ya kufufua soka lake nchini Italia chini ya kocha wa Atalanta Gian Piero Gasperini, alifunga mabao mawili ndani ya dakika 26 za kwanza kabla ya kufunga bao la tatu dakika 15 kabla ya mchezo kumalizika.

Amekuwa mtu wa sita kufunga mabao matatu katika mechi kubwa ya fainali barani Ulaya, na wa kwanza tangu Jupp Heynckes alipoifungia Borussia Moenchengladbach katika fainali ya kombe la UEFA mwaka 1975.

Ushindi huo umehitimisha harakati za Gasperini za miongo miwili akitafuta taji kubwa huku timu yake ya Bergamo pia ikihitimisha subira ya miaka 61, tangu ushindi wao wa kombe la Italia mnamo mwaka 1963.

Atalanta Bergamo - Bayer 04 Leverkusen
Kocha wa Bayer Leverkusen Xabi Alonso akitafakari baada ya kipigo cha kushangaza kutoka kwa Atalanta Bergamo.Picha: Federico Gambarini/dpa/picture alliance

Lakini kama walivyofanya dhidi ya vinara wa Ligi ya Premia, Liverpool na washiriki mara tatu wa fainali hiyo Olympique de Marseille katika raundi mbili za awali, Atalanta hawakuwapa wapinzani wao nafasi ya kuadhimisha fainali yao ya kwanza ya Europa kwa ushindi maarufu.

Soma pia: Leverkusen waangazia macho fainali mbili zilizobaki

Hii ni mara ya pili kwa Leverkusen kushindwa kutwaa taji la bara, kufuatia mafanikio ya 1988 katika michuano hiyo hiyo ambayo wakati huo ilikuwa inaitwa Kombe la UEFA, kama walivyopoteza katika fainali ya Ligi ya Mabingwa wa 2002 dhidi ya Real Madrid.

'Hatuwezi kuruhusu hili lituvunje'

Lakini bado wanaweza kumaliza msimu wakiwa kifua mbele na kusisimua zaidi sherehe kubwa iliyopangwa Jumapili nyumbani, kwa kushinda fainali ya Kombe la Ujerumani Jumamosi mjini Berlin ambapo wanapewa nafasi kubwa zaidi dhidi ya Kaiserslautern ya daraja la pili.

Nahodha wa Bayer Leverkusen Jonathan Tah aliwahimiza wachezaji wa timu yake kutovunjwa moyo na kupoteza fainali ya Ligi ya Europa, na badala yake watumie uchungu huo kushinda Kombe la Ujerumani.

Tah amabye alikabidhiwa kitambaa cha unahodha baada ya nahodha wa kawaida Lukas Hradecky kuwekwa kwenye benchi, aliiambia RTL+ "hatuwezi kuruhusu hili lituvunje".