Afrika yaanzisha kampeni ya kukomesha silaha kufikia 2020
28 Februari 2019Azimio lililopitishwa na baraza hilo linaelezea uungwaji mkono wa juhudi zinazolenga kutafutia ufumbuzi wa kiafrika kwa matatizo ya kiafrika wakati ikitambua kuwa nchi nyingine zinaweza kutia chachu maendeleo hayo. Baraza lilitambua juhudi za Umoja wa Afrika na jumuiya za kikanda za kuwa na bara lisilo na mizozo, lakini pia likielezea "wasiwasi juu ya changamoto za hali ya kiusalama katika baadhi ya maeneo barani Afrika."
Limebainisha vitisho vinavyoletwa na ugaidi, uharamia wa majini, mivutano baina ya wakulima na wafugaji, uhalifu wa nchi moja hadi nyingine, na vurugu zinazochangiwa na wanamgambo, waasi na makundi yaliyo na silaha.
Mwakilishi wa Umoja wa Afrika katika kampeni ya "kutokomeza silaha" Ramtane Lamamra, amesema "hatua kadhaa zimepigwa katika kuzuia, kudhibiti na kusuluhisha migogoro Afrika. Amegusia makubaliano ya amani kama yale ya Sudan Kusini, na Jamhuri ya Afrika ya Kati pamoja na chaguzi zilizofanyika nchini Madagascar na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, sambamba na kufufuka kwa mahusiano baina ya Eritrea na Ethiopia katika pembe ya Afrika.
Lakini mwakilishi huyo, pia alilieleza baraza hilo kwamba "idadi kadhaa ya nchi za kiafrika bado zimekwama katika mzunguko wa mizozo ya vurugu na athari zake". Hakutaja majina lakini Mali na nchi nyingine katika ukanda wa Sahel, pamoja na Congo, Libya, Somalia na Sudan ni mataifa yanayokabiliwa na machafuko na mashambulizi ya wanamgambo na makundi yenye silaha.
Lamamra alisema uhalifu, ugaidi na kuenea kwa silaha ndogo kunachangia shughuli haramu, huku ufisadi usioisha, mzunguko haramu wa fedha na matumizi mabaya ya rasilimali za umma, utawala mbaya ni chanzo kikubwa cha migogoro barani afrika na kukosekana kwa utulivu. "Changamoto hizi zinakwamisha haja ya haraka ya utamaduni wa kuzuia migogoro" alisema mwakilishi huyo.
Naye mkuu wa masuala ya kisiasa na ulinzi wa amani wa Umoja wa Mataifa Rosemary Dicarlo anakubaliana kwamba "changamoto nyingi za kiutawala, kuyatenga makundi fulani kutoka kwenye mchakato wa kisiasa, ufisadi na matumizi mabaya rasilimali za umma ni matataizo yanayopaswa kushughulikiwa kwa pamoja.
Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AP
Mhariri: Josephat Charo