1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa zamani Guinea ashikiliwa kwa saa kadhaa

Grace Kabogo
20 Septemba 2021

Uongozi mpya wa kijeshi nchini Guinea ulimshikilia kwa saa kadhaa waziri wa zamani wa viwanda, Tibou Kamara baada ya kumkamata jana asubuhi na kuipekua nyumba yake.

https://p.dw.com/p/40YKB
Guinea Junta
Picha: Sunday Alamba/AP/picture alliance

Kwa mujibu wa wasaidizi wa Kamara na taarifa rasmi, waziri huyo wa zamani alipelekwa sehemu kusikojulikana bila kutolewa maelezo yoyote.

Kamara pia alikuwa msemaji wa serikali ya Alpha Conde aliyeondolewa madarakani katika mapinduzi ya kijeshi Septemba 5.

Takribani wanaume 10 waliipekua nyumba yake na kuchukua vitu kadhaa ikiwemo simu za wasaidizi wake.

Kamara aliachiliwa huru jana mchana. Kamati ya Kitaifa ya Maridhiano na Maendeleo, CNRD inayotawala Guinea imethibitisha kukamatwa kwa waziri huyo, ikimshutumu kwa kukiuka ahadi ya kutoegemea upande wowote katika uongozi wa kijeshi.

Baada ya mapinduzi, CNRD iliiarifu serikali iliyoondolewa madarakani kutokufanya mawasiliano yoyote ambayo yanaweza kuvuruga amani ya kijamii na ari ya kizalendo iliyoletwa na CNRD.