1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUturuki

Watu wawili waokolewa Uturuki baada ya siku 11

Bruce Amani
17 Februari 2023

Waokoaji nchini Uturuki wamewatoa leo watu wawili wakiwa hai kwenye vifusi vya majengo yaliyoporomoka nchini Uturuki, siku 11 baada ya mkasa wa tetemeko la ardhi.

https://p.dw.com/p/4Nezl
Türkei | Ukrainische Rettungseinheiten in Antakya
Picha: Kyodo News/IMAGO

Mkasa huo wa tetemeko la ardhi umesababisha vifo vya zaidi ya watu 43,000 na kuwaacha mamilioni ya wengine bila makaazi. Misikiti kote ulimwenguni ilisali sala maalumu kwa ajili ya waliokufa nchini Uturuki na Syria.

Huku baadhi ya timu za kimataifa za uokozi zikiwa tayari zimeondoka katika eneo la mkasa, manusura wanaendelea kutolewa kwenye vifusi vya majumba yaliyoporomoka. Katika mji wa Antakya, kijana mmoja mwenye umri wa miaka 14 na mwanaume mwenye umri wa miaka 34 waliokolewa ikiwa ni masaa 260 baada ya kutokea tetemeko hilo.

Umoja wa Mataifa umetoa wito wa kuchangishwa zaidi ya dola bilioni moja kushughulikia operesheni za kiutu nchini Uturuki, siku mbili tu baada ya kutoa ombi la dola milioni 400 kwa ajili ya watu wa Syria.