Watu wajitokeza kwa wingi kupiga kura Misri
16 Desemba 2012Wakati kukiwa na misururu mikubwa katika vituo vya kupigia kura, tume ya uchaguzi imerefusha muda wa upigaji kura kwa saa nne jana Jumamosi(15.12.2012).
Vituo vya televisheni nchini Misri vimeonyesha misururu ya wapiga kura wakiwa bado wanasubiri kupiga kura usiku, bila kujali hali ya baridi kali.
Watazamaji wa uchaguzi huo wamesema kuwa upigaji kura umechafuliwa na ukiukaji mkubwa, ikiwa ni pamoja na upigaji kura wa halaiki, ukosefu wa uangalizi kamili wa majaji pamoja na kufanya ushawishi kinyume na sheria.
Mabadiliko bado
"Aina zote za udanganyifu zilizoonekana katika enzi za rais aliyeondolewa madarakani Hosni Mubarak zimeonekana tena leo," Hafez Abu Saada , mwanaharakati maarufu wa kupigania haki za binadamu , amekiambia kituo cha binafsi cha televisheni cha Dream.
Mubarak aliondolewa kiasi miaka miwili iliyopita.
Mkuu wa tume ya uchaguzi Zaghloul al-Balshi amekana madai hayo kwamba upigaji kura hauangaliwi kwa ukamilifu na majaji.
"Tutatathmini malalamiko yote ili kubaini athari yake kwa uhalali wa mchakato huu," ameuambia mkutano na waandishi habari jana Jumamosi(15.12.2012).
Amesema kuwa matokeo yatatangazwa rasmi baada ya duru ya pili na ya mwisho ya upigaji kura itakayofanyika hapo Desemba 22.
Kura ya maoni yaonesha kuelemea kuidhinishwa
Zoezi la kuhesabu kura limeanza jana Jumamosi (15.12.2012) baada ya kumalizika kwa upigaji kura huku matokeo ya awali yakionesha kuelekea kuidhinishwa kwa kura hiyo ya maoni, vimeripoti vyombo vya habari vya nchi hiyo.
Chama cha rais Mohammed Mursi cha Udugu wa Kiislamu pamoja na washirika wao wamefanya kampeni kwa nguvu ili rasimu hiyo ya katiba iidhinishwe, wakidai kuwa ni muhimu kuharakisha hatua za mpito kutoka utawala wa kiimla wa Mubarak.
Upande wa upinzani unasema kuwa katiba hiyo, iliyoandikwa na baraza linalomilikiwa na vyama vinavyoongozwa na makundi ya Kiislamu , inaweza kukandamiza haki za wanawake na za kisiasa na kuwatenga watu wa makundi ya wachache.
"Sipendi mfumo wa Kiislamu udhibiti nchi yangu kwa sababu nafahamu kuwa Mursi ni dikteta, anadhibiti maisha yangu na ya familia yangu. Napendelea uhuru," Naier al-Guindy, mwenye umri wa miaka 59, ameliambia shirika la habari la dpa katika kituo cha kupigia kura cha Garden City katikati ya mji wa Cairo.
Utata katika rasimu
Hinar Sabry, mwenye umri wa miaka 25 , msichana ambaye amevaa hijabu, amesema kuwa atapiga kura ya ndio kuidhinisha katiba hiyo.
"Vifungu ambavyo watu wanafikiri vina utata kwa kweli havina utata hivyo, wanajaribu tu kuleta mtafaruku juu ya katiba hiyo katika televisheni, amesema msichana huyo.
"Hii inahusu zaidi msimamo wa kisiasa kwa upande wa upinzani. Upinzani unahitaji madaraka tu, na hawajali juu ya kile katiba inachosema."
Mamia kwa maelfu ya wanajeshi na polisi wamewekwa nje ya vituo vya kupigia kura ili kulinda usalama. Mshindi wa nishani ya amani ya Nobel Mohammed ElBaradei, ambaye anaongoza muungano wa upinzani wa National Salvation Front , amehimiza kura ya "HAPANA ".
Hapo kabla amemtaka rais Mursi kuahirisha kura hiyo ya maoni, akionya kuwa kunaweza kutokea vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Mwandishi : Sekione Kitojo / dpae
Mhariri: Iddi Ismail Ssessanga