1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waandishi habari waliofariki ajalini waagwa Mwanza

Dotto Bulendu12 Januari 2022

Miili ya waandishi habari waliofariki katika ajali ya barabarani mkoani Simiyu, Tanzania, imeagwa katika uwanja wa Nyamagana makoani Mwanza, katikati mwa vilio na huzuni huku waajiri wakiagizwa kulipa mafao yao haraka.

https://p.dw.com/p/45RPU
Tansania Mwanza | Trauer um ITV Journalist Husna Mlanzi
Picha: Dotto Bulendu/DW

Asubuhi kulipambazuka huku kukiwa kumetawaliwa na ukimya katika maeneo mbalimbali ya jiji la Mwanza kufuatia vifo hivyo vya waandishi wa habari walioagwa hii leo na mamia ya watu waliojitokeza katika uwanja wa mpira wa miguu wa Nyamagana wakiongozwa na waziri wa habari, mawasiliano na teknolojia ya habari Nape Nnauye.

Wanahabari hao ni sehemu ya watu 14 waliofariki dunia baada ya gari la waandishi wa habari iliyokuwa kwenye msafara wa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza (RC), Robert Gabriel kugongana na gari ya abiria aina ya Toyota Hiace katika eneo la Nyamikoma, Wilaya ya Busega katika Mkoa wa Simiyu.

Tansania Mwanza | Trauer um ITV Journalist Husna Mlanzi
Waombolezaji wakiuaga mwili wa aliekuwa aifa habari wa mkoa wa Mwanza Abel Ngapemba.Picha: Dotto Bulendu/DW

Waandishi wa habari walipoteza maisha katika ajali hiyo ni Husna Mlanzi kutoka kituo cha televisheni cha ITV, Vanny Charles (Icon), Antony Chuwa, Johari Shani (Uhuru Digital) na Abel Ngapemba ambaye ni Afisa Habari Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.

Waajiri wapewa siku saba kulipa stahiki za marehemu

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye na viongozi wengine wamewaongoza waombolezaji wakiwemo wanahabari, ndugu na jamaa wa familia waliofiwa kutoa heshima za mwisho kabla ya kila mwili kuzikwa katika eneo lake.

Waziri Nape ametumia jukwaa hilo kuagiza viongozi wa serikali kuweka mazingira bora  yatakayowawezesha wanahabari kufanya kazi kwa usalama, huku akiwataka pia waajiri wanaodaiwa na waandishi wa habari waliofariki katika ajali ya gari wilayani Busega kulipa stahiki zao.

"Nimepewa salamu hapa kuwa miongoni mwa waliolala kwenye majeneza hapa mbele yangu hawajalipwa stahiki zao; natoa siku saba kwa waajiri wote wanaodaiwa kulipa stahiki zote za marehemu na kutoa taarifa ofisi ya mkuu wa mkoa," alisema Nape.

Tansania Mwanza | Trauer um ITV Journalist Husna Mlanzi
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Robert Gabriel akizungumza na waziri wa habari, mawasiliano na teknolojia NApe Nnauye wakti wa shughuli ya kuaga miili ya waandishi habari waliofariki katika ajali tarehe 11, 01, 2022 mkoani Simiyu.Picha: Dotto Bulendu/DW

Awali, wawakilishi wa waandishi wa habari waliotoa salamu walimuomba waziri huyo kushughulikia changamoto ya waandishi kutolipwa stahiki zao huku wakifichua kuwa baadhi ya marehemu hawajalipwa kwa miaka miwili iliyopita.

Waliozungumza kwa niaba ya wanahabari ni Mwenyekiti wa Kluabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mwanza (MPC), Edwin Soko na Mkurugenzi mtendaji wa Klubu ya Waandishi wa Habari (UTPC), Abubakar Karsan.