1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchunguzi dhidi ya shirika la misaada la UNRWA waanza

Zainab Aziz
14 Februari 2024

Jopo la wataalamu huru linapanga kuanza kulichunguza shirika la Umoja wa Mataifa linalotoa misaada kwa wakimbizi wa kipalestina,(UNRWA) baada ya Israel kutoa madai mazito dhidi ya shirika hilo.

https://p.dw.com/p/4cP6N
Ukanda wa Gaza | Shirika la misaada la UNRWA
Wanajeshi wa Israel wakiwa nje ya jesho la shirika la misaada la UNRWA GazaPicha: JACK GUEZ/AFP/Getty Images

Umoja wa Mataifa umelianzisha jopo hilo chini ya uongozi wa aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa Catherine Colonna, ambaye atashirikiana na wataalamu wa taasisi za Sweden, Norway na nyingine ya haki za binadamu ya Denmark.

Ripoti ya awali inatarajiwa kutolewa mwishoni mwa mwezi wa Machi. Shirika la misaada la Umoja wa Mataifa UNRWA limegonga vichwa vya habari hivi karibuni baada ya Israel kutoa madai kwamba watumishi kadhaa wa asasi hiyo walijihusisha na vitendo vya kigaidi vya tarehe 7, Oktoba mwaka uliopita wakati kundi la Hamas lilipofanya mashambulizi dhidi ya Israel.

Soma pia:UNRWA yangoja ripoti uhusika wa watumishi shambulio la Oktoba 7

Kutokana na madai hayo nchi kadhaa za magharibi ikiwa pamoja na wafadhili wakubwa kabisa Marekani na Ujerumani zilisimamisha misaada ya fedha kwa ajili ya shirika hilo la Umoja wa Mataifa.