Uchaguzi tete wa mageuzi ya katiba Komoro
30 Julai 2018
Baadhi ya vituo vya kupiga kura vimekawia kufunguliwa. Idadi ndogo kabisa ya wapiga kura wanaonekana kuteremka vituoni asubuhi ya leo katika mji mkuu wa Komoro Moroni.
Machafuko yameripotiwa katika baadhi ya vituo vya kupiga kura katika mji mkuu wa Komoro-Moroni ambako mwanajeshi mmoja amekatwa mkono na kundi la watu wasiojulikana. Katika kisiwa cha Nzuwani pia kuna ripoti zinazosema risasi zilifyetuliwa jana usiku kuamkia leo katika ya mji wa Wani.
+Upande wa upinzani wapinga kura ya maoni ya katiba
Visiwa hivyo vya bahari ya Hindi vilivyowahi kukumbwa na mitihani ya mapinduzi, vinakabiliwa na hatari ya kutumbukia upya katika janga la machafuko baada ya rais Assoumani kupiga marufuku maandamano huku upande wa upinzani ukipania kupinga kwa kila hali mageuzi yaliyopendekezwa.
Wabunge wa upande wa upinzani wametoa wito wa kusitishwa "bila ya masharti zoezi hilo la kura ya maoni wanalolitaja kuwa "la kiimla na kinyume na sheria" zoezi wanalosema limeandaliwa makusudi kukidhi malengo ya rais.
Lakini waziri wa mambo ya ndani Mohammed Daoud amepinga madai ya upande wa upinzani na kusema wapiga kura laki tatu waliosajiliwa watakwenda kupiga kura.
Kuambatana na katika ya sasa iliyoidhinishwa mwaka 2001, madaraka yanazunguka kila baada ya miaka 5 kati ya visiwa vitatu kati ya vinne vya bahari ya Hindi, Ngazija, Nzuwani na Mwali-lengo likiwa kuhakikisha madaraka sawa kati ya visiwa hivyo.
Pindi serikali ikiibuka na ushindi, utaratibu huo utasitisahwa na badala yake madaraka kudhibitiwa na rais atakaechaguliwa kwa mhula wa miaka mitano unaoweza kurefushwa mara moja.
Rais Azali Assoumani atuhumiwa kuhodhi madaraka
Rais Assoumani atakuwa pia na madaraka ya kuwafuta kazi makamo watatu wa rais-nguzo nyengine ya wezani sawa wa madaraka inayodhaminiwa na katiba ya mwaka 2001.
Mwezi uliopiota , mmojawapo wa makamo wake wa rais Ahmed Said Jaffar aliwatolea wito wakomoro wasiunge mkono kile alichokiita" "matumizi mabaya ya madaraka. Wito huo ukawa sababu ya kupokonywa nyadhifa zote serikalini isipokuwa mmoja tu.
Pindi Assoumani akiibuka na ushindi, anatarajiwa kuitisha uchaguzi wa rais mwakani, miaka miwili kabla ya wakati. Kwa mujibu wa msemaji wake, Mohammed Ismaila, pindi akishindwa atang'atuka.
Azali Assoumani ameshawahi kuvitawala visiwa vya Komoro kati ya mwaka 1999 na 2002 baada ya mapinduzi ya kijeshi dhidi ya rais wa muda Tadjiddine Ben Said Masdoud. Alishinda kwa mara ya kwanza uchaguzi wa vyama vingi mwaka 2002 na kumkabidhi madaraka rais aliyechaguliwa na wananchi mwaka 2006 Ahmed Abdallah Sambi. Azali Assoumami amerejea tena madarakani mwaka 2016 kufuatia uchaguzi uliogubikwa na visa vya udanganyifu. Mwezi April mwaka huu ameivunja korti ya katiba akihoji haina uwezo.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP
Mhariri:Yusuf saumu