1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano yamalizika.

Abdu Said Mtullya14 Aprili 2009
https://p.dw.com/p/HWrq
Wanajeshi waliotishia kutumia nguvu dhidi ya wapinzani wa serikali.Picha: AP


Polisi ya Thailand imewafungulia mashkata  viongozi watatu  wa maandamano yaliyofanyika kuipinga serikali, yaliyomalizika leo baada ya wanajeshi kutishia kutumia nguvu. 

Wakati huo huo mahakama  imetoa hati ya kisheria ya kuwezesha kukamatwa kwa aliekuwa waziri mkuu wa Thailand Thaksin Shinawatra  anaeishi nje ya nchi hiyo.

Waranti juu ya kukamatwa kwa bwana Shinawatra  umetolewa  pia kwa watu wengine 12 wanaomuunga  mkono waziri mkuu huyo wa  zamani.

Kufunguliwa mashtaka kwa viongozi hao watatu - wapinzani wa serikali ya Thailand, pamoja na waranti uliotelewa dhidi ya bwana Shinawatra kunafuatia kumalizika leo, kwa maandamano na harakati za kuipinga serikali ambapo wapinzani  waliweza  kuyadhibiti  makao makuu ya serikali kwa muda  wa takriban wiki tatu.

Kwa mujibu wa waranti uliotolewa , Shinawatra na watu  wanaomuunga mkono  wamechochea  ghasia,  na wamehatarisha amani; adhabu ya makosa hayo ni  kifungo cha miaka mitano jela.

Katika maandamano ya kuipinga serikali yaliyochukua takriban wiki tatu, nchini Thailand watu wawili waliuawa na wengine 123  wamejeruhiwa.

Wapinzani wa serikali wanaomuunga mkono waziri  mkuu wa  zamani Shinawatra  walipambana na  wanajeshi .

Lakini mvutano huo umemalizika kwa amani na mji  mkuu Bangkok umerejea katika utulivu kidogo.

Mwandishi:Mtullya.

Mhariri:Abdul-Rahman.

AFP.