Suluhisho la kisiasa Syria
15 Oktoba 2015Alaeddin Boroujerdi mkuu wa kamati ya bunge ya usalama wa taifa nchini Iran akizungumza na waandishi wa habari mjini Damascus Alhamisi (15.10.2015) amesema Iran itazingatia suala la kutuma vikosi vyake nchini Syria iwapo serikali ya nchi hiyo itatowa ombi hilo.
Amesema "Tumetangaza mara kwa mara na leo ninasema tena kwamba sluhisho pekee la kuutatuwa mzozo wa Syria ni suluhisho la kisiasa tu.Juhudi zozote zile ambazo hazijumuishi uratibu na serikali ya Syria haziwezi kufanikiwa."
Boroujerdi mkuu wa kamati hiyo ya bunge yenye ushawishi mkubwa katika masuala ya usalama wa taifa na sera za kigeni nchini Iran amesisitiza uungaji mkono kikamilifu wa serikali yake kwa Syria na kwamba suluhisho la kisiasa ndio njia pekee ya kuondokana na mzozo huo uliopo hivi sasa.
Kauli yake hiyo inakuja siku moja baada ya afisa mmoja wa kanda hiyo kusema kwamba mamia ya wanajeshi wa Iran wanawekwa kaskazini na kati ya Syria na hiyo kuzidisha kujihusisha kwa Iran katika vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Syria kwa kusaidiana na wapiganaji wa Hezbollah wa Lebanone na mashambulizi ya anga ya Urusi kufanya shambulio kuu la kuyakombowa maeneo yaliotekwa na waasi.
Maafisa wa Iran na Syria walikuwa tayari wamekiri kwa muda mrefu kwamba Iran ina wshauri na wataalamu wa kijeshi nchini Syria lakini wamekanusha uwepo wowote ule wa wanajeshi wake wa nchi kavu nchini humo.
Suluhisho la kisiasa
Akizungumza katika kikao cha bunge la Ujerumani Jumatano (14.10.2015) waziri wa mambo ya nje Frank Walter Steinmeir pia amesisitiza haja ya kufikiwa suluhisho la kisiasa kukomesha mzozo huo wa miaka minne nchini Syria na kwamba Urusi inahitajika kufanikisha suluhisho hilo
Steinmeier amekaririwa akisema "Hakuna mtu anayeweza kufanikisha hilo pekee yake. Tunahitaji kila mtu kwa hili. Hususan washirika wa kanda majirani kama vile Uturuki na Iran halikadhalika Saudi Arabia. Tunaihitaji Ulaya.Tunaihitaji Marekani.Lakini kwa kuzingatia mazingira ya siku mbili tatu zilizopita na yale ya wiki za karibuni tunajuwa pia kwamba hilo haliwezekani bila ya kujumuishwa kwa Urusi."
Urusi imeanza mashambulizi yake ya anga nchini Syria hapo Septemba na 30 vikosi vya serikali ya Sria na wanamgambo washirika vilianzisha shambulio la ardhini kati kati ya Syria wiki moja baadae.
Mwandishi : Mohamed Dahman /AP/dpa
Mhariri : Yusuf Saumu