Snowden akataa masharti ya Urusi
2 Julai 2013Raia huyo wa Marekani Edward Snowden mwenye umri wa miaka 30, ambaye anakabiliwa na kesi ya kufanya ujasusi dhidi ya nchi yake, ameomba hifadhi ya kisiasa katika nchi 15 na anaendelea kuwapo katika eneo linalotumiwa na wasafiri kusubiri kuendelea na safari zao katika uwanja wa ndege wa mjini Moscow wa Sheremetyevo.
"Mtu kuomba hifadhi ya kisiasa akiwa hayupo katika nchi anayotaka kuishi , kimsingi haikubaliki," naibu waziri wa sheria wa Norway Paal Loenseth ameliambia shirika la habari la nchi hiyo NRK.
"Ombi la hifadhi ya kisiasa ni lazima lifanywe katika ardhi ya Norway. Kwa mujibu wa utaratibu wa kawaida , ombi lake litakataliwa."
Hapo mapema wizara ya mambo ya kigeni imesema kuwa imepokea ombi kwa ajili ya hifadhi ya kisiasa kutoka kwa Snowden kwa njia ya fax katika ubalozi wake mjini Moscow mchana jana Jumatatu.
Wakati huo huo , "Snowden aliomba kuendelea kuishi nchini Urusi , lakini jana , baada ya kufahamu msimamo wa rais Putin kulingana na masharti ambayo anaweza kuishi nchini humo, aliondoa ombi lake," amesema msemaji wa rais Putin , Dmitry Peskov.
Snowden hataki masharti
"Kimantiki , Snowden anaweza kuishi katika shirikisho la Urusi kwa masharti kuwa anaachana na shughuli zake za kufichua taarifa za siri za Marekani. Kwa mujibu wa yale tunayoyafahamu , hataki kuachana na shughuli hizo, ameongeza msemaji huyo wa rais. Rais Putin amesema.
"Iwapo anataka kwenda kokote na atapokelewa huko anakotaka kwenda, tuko tayari kumruhusu. Iwapo anataka kubaki hapa nchini, tuna sharti moja; ni lazima aachane na shughuli zake zenye lengo la kuwadhuru washirika wetu, licha ya kuwa inaonekana si jambo la kawaida kwamba mimi ndio natamka maneno hayo."
Anakabiliwa na vikwazo kadha
Poland imekataa pia kumpokea Snowden , wakati maafisa nchini Ujerumani , Austria na Uswisi wamesema kuwa hawezi kupeleka maombi yake katika nchi hizo wakati yuko katika nchi nyingine.
Tovuti inayofichua taarifa za siri ya Wikileaks imesema kuwa Snowden , ambaye anaamika kuwa yuko katika uwanja wa ndege mjini Moscow , ameomba hifadhi ya kisiasa katika nchi zipatazo 21 ikiwa ni pamoja na nchi 13 katika bara la Ulaya. Mataifa mengi ya Ulaya yanataka ombi kama hilo kufanywa katika ardhi ya nchi hizo na sio nje.
Rais wa Venezuela Nicolas Maduro amesema leo kuwa Edward Snowden , anastahili "ulinzi wa dunia" kwa kutoa taarifa za mpango wa ujasusi wa Marekani.
Mwandishi : Sekione Kitojo / rtre / ape
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman