1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaKorea Kusini

Putin atoa wito wa ushirikiano zaidi na Korea Kaskazini

Tatu Karema
9 Septemba 2023

Rais wa Urusi Vladmir Putin ametoa wito wa kuimarisha ushirikiano katika nyanja zote na Korea ya Kaskazini, wakati akimpongeza kiongozi wa taifa hilo Kim Jong Un kwa kuadhimisha miaka 75 tangu kuanzishwa kwa taifa lake

https://p.dw.com/p/4W8mY
Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un akitoa hotuba wakati wa hafla ya uzinduzi wa nyambizi mpya ya mashambulizi ya nyuklia mnamo Septemba 6, 2023
Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong UnPicha: uncredited/KCNA via KNS/AP/picture-alliance

Maadhimisho hayo yaliyoanza Ijumaa usiku yamefanyika wakati kukiwa na matarajio kuwa Kim Jong Un atasafiri kwenda Urusi hivi karibuni kukutana na Rais Putin. Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na ujumbe kutoka China ukiongozwa na naibu wa waziri mkuu, Liu Guozhong wakati Urusi ikiwa imetuma kikundi cha dansi na wimbo wa kijeshi.

Korea Kusini yasema kuna maandalizi ya mkutano kati ya Kim na Putin 

Vyombo  vya habari vya Korea Kusini vinatilia shaka kuwa, kukosekana kwa wawakilishi wa serikali ya Urusi kwenye mkutano huo kuna uhusiano na maandalizi ya mkutano kati ya Kim na Putin ambao huenda ukafanyika wiki ijayo. Mkutano huo huenda ukajikita katika mauzo ya silaha za Korea Kaskazini kwa Urusi, ili kuongeza akiba ya silaha ya Kremlin ambayo imepungua kutokana na vita  dhidi ya Ukraine.