Podolski hatacheza hadi mwisho wa mwaka
4 Septemba 2013Jeraha kwenye goti alilolipata mchezaji wa safu ya mashambulizi ya timu ya taifa ya Ujerumani, Lukas Podolski, ni baya zaidi kuliko ilivyohofiwa hapo awali. Hii ina maana mshambuliaji huyo wa klabu ya Arsenal London hatacheza hadi mwezi Desemba mwaka huu.
Daktari wa timu ya taifa ya kandanda ya Ujerumani, Hans-Wilhelm Mueller-Wohlfahrt, amemfanyia uchunguzi Podolski mjini Munich na kugundua amekatika ukano wa mvungu wa goti la mguu wake wa kushoto. "Kwa bahati mbaya sitaweza kucheza kwa muda mrefu, kama miezi mitatu," Podolski ameliambia gazeti la kila siku la Ujerumani, Bild.
Podolski atakosa mechi za kufuzu kwa kombe la dunia la kandanda nchini Brazil mwakani zilizosalia mwaka huu. Alitolewa uwanjani akiwa kwenye machela dakika ya 50 ya mechi kati ya klabu yake ya Arsenal na Fernerbahce Istanbul wiki iliyopita, wakati ilipofikiriwa angekuwa nje ya uwanja bila kucheza mechi yoyote kwa wiki hadi 10.
Mwandishi: Josephat Charo/APE
Mhariri: Iddi Sessanga