1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matumaini ya chanjo, virusi vya corona Ujerumani yaongezeka

13 Agosti 2020

Waziri wa afya wa Ujerumani Jens Spahn amesema leo kuwa ana matumaini ya kupatikana kwa chanjo ya virusi vya corona katika miezi michache ijayo na hasa mwaka ujao.

https://p.dw.com/p/3gtGY
Coronavirus Impfstoff Symbolbid
Picha: picture alliance/AP Photo

Kauli hiyo ya Spahn inakuja baada ya Taasisi ya Robert Koch nchini Ujerumani kukanusha ripoti ya awali kwamba kutakuwa na chanjo tayari katika msimu wa mapukutiko. Taasisi hiyo imesema kwamba ripoti hiyo ilikuwa haijakamilishwa na kwamba ilichapishwa kimakosa. Waziri Spahn lakini hakutoa mwezi kamili ambao chanjo hiyo itakuwa tayari.

Je, ni mara ngapi watu watahitajika kutumia chanjo?

Deutschland | Gesundheitsminister Spahn |  Corona-Testpflicht für Rückkehrer aus Risikogebieten
Waziri wa Afya wa Ujerumani Jens SpahnPicha: picture-alliance/dpa/AFP/T. Schwarz

Anasema bado haijabainika ni mara ngapi watu watahitajika kupewa chanjo hiyo au kinga ya chanjo hiyo itadumu kwa muda gani mwilini. Waziri wa utafiti wa Ujerumani Anja Karliczek awali alisema kwamba hakuna uwezekano wa chanjo yoyote kutolewa kwa umma kabla katikati ya mwaka ujao.

Aidha kwa upande wake Rais Vladimir Putin ametangaza kwamba taifa lake limekuwa la kwanza kupata idhini ya kisheria ya chanjo ya COVID-19 baada ya kufanya majaribio ya kipindi kisichozidi miezi miwili. Lakini  Waziri Spahn amerejea kuonesha mashaka yake juu ya chanjo hiyo, iitwayo "Sputnik V", akisema haijawahi kufanyiwa vipimo vya kina kama ilivyo kwa chanjo nyingine na aina taarifa za kina kuhusu matokeo yake.

Soma zaidi:Chanjo ya Urusi dhidi ya COVID-19 yatiliwa shaka

Kwa mujibu wa taasisi ya Robert Koch (RKI) idadi ya maambukizi nchini Ujeruamani imeongezeka kwa kiasi ya watu 1,445 na kufanya idadi jumla ya 219,964 wakati idadi ya waliokufa imefikia 9,211, baada ya kuongezeka watu wanne.