1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yatoa chanjo ya kuzuia maambukizi ya VVU Afrika

18 Novemba 2025

Marekani imesema leo kuwa imetoa chanjo mpya ya kuzuia maambukizi ya virusi vya Ukimwi kupitia dawa ya Lenacapavir katika nchi mbili za Afrika.

https://p.dw.com/p/53oeP
Afrika Kusini 2024 | Uzuiaji wa VVU kupitia dawa ya Lenacapavir
Dawa ya Lenacapavir inayotumika katika tiba mpya ya kuzuia VVUPicha: Nardus Engelbrecht/AP Photo/picture alliance

Mkurugenzi mtendaji wa Global Fund, Peter Sands, amesema kwa ujumla, takriban dozi 1,000 zimewasilishwa nchini Eswatini na Zambia na zitaanza kutolewa wiki hii.

Marekani inapanga kupanua usambazaji wa chanjo hiyo ya Lenacapavir kwa kufanya kazi na kundi la kimataifa, Mfuko wa Kimataifa wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria, pamoja na kampuni ya dawa ya Sayansi ya Gileadi.

Juhudi za kusambaza tiba ya kuzuia VVU kupanuliwa kwengineko Afrika

Mwenyekiti na Mkurugenzi Mtendaji wa Gileadi Daniel O'Day, amesema juhudi zinaendelea ili kuidhinisha usambazaji wa dawa hiyo ya Lenacapavir katika nchi za Botswana, Kenya, Malawi, Rwanda, Namibia, Tanzania na Zimbabwe.

Pia ameongeza kuwa huu ni wakati muhimu sana katika historia ya VVU na mara ya kwanza kwa dawa kutolewa barani Afrika mwaka ambao imeidhinishwa Marekani.