Manchester City yapunguza pengo na Chelsea
1 Desemba 2014Mabingwa Manchester City iliendelea kujiimarisha na kusonga hadi nafasi ya pili kutokana na ushindi wa mabao matatu kwa sifuri dhidi ya Southampton. Mahasimu wengine wa Chelsea -- Manchester United ambao waliwazaba Hull mabao matatu kwa sifuri, Arsenal waliowashinda West Bromwich Albion goli moja kwa sifuri, na Liverpool waliowafunga Stoke goli moja kwa sifuri, bila shaka walikuwa na kila sababu ya kuwashukuru Sunderland kwa kazi walioifanya.
Katika Ligi ya Ufaransa, Oympique de Marseille inaendelea kuongoza kufuatia ushindi wa mabao mawili kwa sifuri dhidi ya Nantes. Marseille wako mbele ya Paris St Germain kwa tofauti ya point moja baada ya PSG kupata ushindi wa bao moja kwa sifuri dhidi ya Nice. Monaco ilipata kipigo kingine baada ya kunyamazishwa magoli mawili kwa sifuri katika uwanja wa Rennaisna sasa wako katika nafasi ya kumi na pengo la points 14 dhidi ya nambari moja.
St Etienne hatimaye ilifaulu baada ya miaka 20 kumpiku hasimu wake Olympique Lyonnais, ambaye yuko katika nafasi ya tatu. Nchini Italia, Juventus na AS Roma zilishinda mechi zao na kuwacha pengo baina yao kileleni mwa ligi kuwa points tatu. Juve iliishinda Torino mabao mawili kwa sifuri, wakati Roma ikiishinda Inter Milan mabao manne kwa mawili.
Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/reuters
Mhariri: Josephat Charo