Maoni ya wahariri.
4 Machi 2008
Chama cha Social Demokratik kilichomo
katika serikali ya mseto hapa nchini
Ujerumani kinakabiliwa na mtihani baada
ya baraza kuu la chama hicho kutoa
idhini kwa matawi yake juu ya kuweza
kushirikiana na chama cha wakomunisti
wa zamani -Die Linke.
Wahariri wa magazeti wanatoa maoni yao juu ya suala hilo.
Gazeti la RHEIN-NECKAR-ZEITUNG kutoka mji wa Heidelberg linasema mwenyekiti wa chama cha SPD Kurt Beck amefikia uamuzi huo kutokana na mshtuko unaosababishwa na uhafifu wa uzalendo. Chama cha SPD kina wasiwasi mkubwa juu ya kupoteza mtu mwenye mvuto wa uongozi.Mwenyekiti Beck anatambua hilo vyema.
Mhariri wa gazeti la FRANKFURTER RUNDSCHAU anakubaliana na tathmini hiyo kwa kusema chama cha Social Demokratik kinasibika kutokana na kutokuwapo uwazi katika uhusiano wake na chama cha wakomunisti wa zamani. Gazeti linaeleza kwamba ,mjadala juu ya uhusiano baina ya SPD na wakomunisti hao ni jambo muhimu,litakalokuwa na manufaa katika mustakabali wa chama hicho.
Mwenyekiti wa SPD Kurt Beck ametambua umuhimu huo wakati mujarabu, kwani anajua ,viongozi wa matawi ya chama katika majimbo na mikoa wapo pamoja nae, na kwa hiyo asilani hakubali kutikiswa.
Gazeti la KIELER NACHRICHTEN lina mtazamo tofauti.Linasema bwana Beck anajipalia makaa kutokana na sera yake juu ya wakomunisti wa zamani.
Mhariri wa gazeti hilo anasema kuwa kwa sasa hakuna anaetamka kwa sauti kubwa ndani ya chama chake, lakini wengi wanajua kwamba ndoto yake ya kuwa Kansela wa Ujerumani sasa inaweza kuenda ajua.
Gazeti linaeleza kuwa ikiwa mwenyekiti huyo wa SPD atashikilia msimamo wake juu ya chama cha mlengo wa kushoto, atateleza kwenye uchaguzi wa chama mwaka ujao.
Na huo ndio utakuwa mwisho wa chama cha umma kama SPD.
Sababu ni kwamba wapigakura za hasira wataona bora kuwapigia kura akina mlengo wa kushoto nawajue moja, badala ya kukipigia kura chama ambacho kwa wakati mmoja kimo serikalini na katika upinzani.
Mhariri wa gazeti la EXPRESS anasema chama cha Social Demokratik sasa kinakabiliwa na mgogoro mkubwa na kwa kweli hali siyo nzuri ndani ya chama hicho.
Mhariri huyo anaeleza kuwa hata mwanadiplomasia kama waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani bwana Steinmeier ambae pia ni makamu mwenyekiti wa chama hicho anakiri kuwa chama chake kinakabiliwa na mtihani. Gazeti linasema chama hicho kimegawanyika kwa kiwango kikubwa.Na mtihani wa mwisho utakuwa katika jimbo la kati la Ujerumani Hesse. Kushirikiana na wakomunisti wa zamani ama la, katika jimbo hilo.