1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Liverpool yaizidi nguvu Tottenham na kurejea kileleni

1 Aprili 2019

Kinyang'anyiro kikali kileleni mwa ligi kinarejea katikati ya wiki hii ambapo mpira sasa upo kwenye uwanja wa Manchester City. City wako nyuma ya Liverpool na pengo la pointi mbili tu

https://p.dw.com/p/3G1y7
Champions League - Jürgen Klopp und Virgil van Dijk
Picha: picture-alliance

Mabingwa watetezi City na Liverpool wamekuwa wakibadilishana nafasi ya kileleni katika wiki chache zilizopita ambapo hakuna timu iliyoweza kujiimarisha katika nafasi ya kwanza. City waliwazaba Fulham 2 – 0 Jumamosi na kuwapiku Liverpool, lakini nao vijana hao wa Jurgen Klopp wakawapiga Tottenham Hotspur 2 – 1 Jumapili na kurudi tena kileleni.

City wako nyuma na mwanya wa pointi 2 lakini wana mechi moja ya ziada, ambayo itapigwa Jumatano watakapowaalika Cardiff City.

Kuna pointi moja tu inayotenganisha nambari tatu Tottenham (pointi 61) na nambari sita Chelsea (pointi 60) katika nafasi mbili za mwisho za kucheza kandanda la Champions League. Na hayo huenda yakabadilika baadaye leo wakati nambari tano Arsenal (pointi 60) watawaalika Newcastle. Manchester United (pointi 61) kisha watacheza na Wolverhampton Jumanne, wakati Chelsea ikiwaalika Brighton na Tottenham wakizindua rasmi uwanja wao mpya dhidi ya Crystal Palace.

Serie A

Na sio England tu ambapo mambo yanatokota. Nchini Italia mapambano yatakuwa makali katika mechi za katikati ya wiki hii, wakati timu zaba zikitafuta pointi muhimu za kucheza kandanda la Ulaya katika sehemu ya mwisho ya msimu uliotawaliwa na mabingwa watarajiwa Juventus.

Inter Milan, AC Milan na Roma zinalenga kujinyanyua baada ya vichapo vya wikendi katika Serie A. huku zikiwa zimesalia mechi tisa, Inter wako nafasi ya tatu baada ya kufungwa 1 – 0 Jumapili na Lazio, wakati AC Milan ambao walifungwa pia 1 -0 na Sampdoria wakiwa nyuma yao na pengo la pointi mbili na wanajaza nafasi ya nne na ya mwisho ya Champions League

Roma wakati huo huo wameanguka hadi nafas ya saba baada ya kubamizwa 4 – 1 nyumbani dhidi ya Napoli. Milan watakwaruzana kesho Jumanne na Udinese. Vinara Juve watacheza dhidi ya Cagliari, huku nambari mbili Napoli ambao wana mwanya wa pointi 15 wakicheza dhidi ya Empoli. Roma watacheza Jumatano dhidi ya Fiorentina