1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Liverpool kukabidhiwa kombe lililiwaponyika miaka 30 sasa

Sekione Kitojo
20 Julai 2020

Liverpool itakabidhiwa rasmi kombe la ubingwa wa England baada  ya kulikosa kwa miaka  30 katika  wiki  ya  mwisho ya Premier League, nafasi za kucheza vikombe  vya Ulaya pamoja  na kushuka daraja pia zitaamuliwa.

https://p.dw.com/p/3fbli
Fußball Premier League FC Liverpool Crystal Palace Jubel
Picha: picture-alliance/Solo Syndication/K. Quigley

Liverpool haihitaji  tena  kusaka  pointi  za  ligi nchini  England lakini kukabidhiwa  taji  lao  la  kwanza  la  Premier League  siku  ya Jumatano katika  uwanja wao  wa  Anfield itakuwa  tukio lenye  hisia kali kwao  pamoja  na  mashabiki  wao. Premier League  inakunja janvi wiki hii , Juventus Turin  itanyakua  taji  lake  la  tisa  mfululizo la Serie A  iwapo  itashinda  michezo  yake  mitatu  katika  muda  wa siku  saba, wakati  huo  huo nchini  Ufaransa  taratibu shughuli viwanjani  zinaanza  kurejea  kwa  mtanange wa  fainali  ya  kombe la  nchi  hiyo  kati  ya  Paris Saint-Germain  na  St Etienne  siku  ya Ijumaa.

UK Liverpool-Fans feiern Meisterschaft
Sherehe zilianza hata hivyo mara baada ya kufahamika kwamba Liverpool ni mabingwa kabla ya msimu kumalizika..Picha: picture-alliance/empics/P. Byrne

nahodha  wa  Liverpool Jordan Hernderson  huenda   ni  majeruhi lakini  atakuwa  tayari  kulinyanyua  juu  kombe  la  ubingwa  wa  ligi siku  ya  Jumatano na  sherehe  maalum katika  uwanja  wa  Anfield zitafanyika  baada  ya  mchezo  dhidi  ya  Chelsea.

Hapa  Ujerumani  machampioni  wa  Bundesliga  mara  nane mfululizo  Bayern Munich  pamoja  na  RB Leipzig wanarejea  katika kambi  za  mazowezi  baada  ya  wiki  kadhaa  za  mapumziko  baada ya  msimu  wa  ligi  ya  Ujerumani  kumalizika  mwishoni  mwa  mwezi uliopita.

Leipzig tayari  wanafahamu  watapambana  na  Atletico Madrid katika  awamu  ya  robo  fainali  ya  michuano  hiyo itakayofanyika kwa  mfumo  wa mtoano mjini Lisbon, wakati  Bayern itabidi  kwanza kukamilisha  kazi  ya  awamu  ya  timu  16  dhidi  ya  Chelsea, baada ya  kushinda  mchezo  wa  mkondo  wa  kwanza  kwa  mabao 3-0.

Fußball Premier League FC Liverpool gewinnt englische Meisterschaft
Kocha wa Liverpool Jurgen KloppPicha: picture-alliance/dpa/PA/P. Byrne

Manchester United  inapaswa  kumbadilisha  mlinda  mlango wake David de Gea  na kumpa nafasi  mlinda  mlango  mwingine  Dean Henderson msimu  ujao, mshambuliaji  wa  zamani   wa  timu  ya taifa  ya  Uingereza  Alan Shearer alisema  baada  ya  Mhispania De Gea  kufanya makosa  kuonesha  mchezo  wa  kukatisha  tamaa katika  kipigo  cha   mabao 3-1 katika  nusu  fainali  ya  kombe  la AF jana  Jumapili dhidi  ya  Chelsea, na kuwa  gumzo la  mashabiki na  viongozi  nchini  Uingereza.

Champions League Barcelona gegen Manchester United |
David de Gea mlinda mlango wa Manchster Unitec aliyesababisha gumzo kuhusu uwezo wake Picha: Reuters/S. Perez

Mlolongo wa makosa

Mlolongo  wa  makosa  aliyofanya  De Gea umesababisha  miito ya kutaka  kumbadilisha  kutoka  chaguo la  kwanza  na  kumsimamisha Henderson katika  lango la  Manchester, baada  ya  kuonesha umahiri  akilinda  lango  la  Sheffield United.

Lakini  kocha  wa  Chelsea Frank Lampard  alimtetea  De Gea  kwa kusema:

"Sio kwasababu  namheshimu  sana De Gea kama  mlinda  mlango. Nafahamu  watu  kila  mara  watamshambulia  mlinda  mlango  wakati akifanya  makosa  kama  yale, kwasababu  wanamkosoa. Lakini  kile nilichofanya  ni  kumwambia Mason Mount wakati  wa  mapumziko kwamba  nataka  kuona  akipiga  mashuti kuelekea golini  zaidi. Alipiga  shuti moja kipindi cha  kwanza , alijaribu kama kuupiga kwa kuuzungusha na  kwangu  mimi, unapaswa  kujaribu nje  ya  box dhidi ya  walinda  mlango wa kiwango cha  juu, na  De Gea  ni  mlinda mlango wa kiwango cha juu, unapaswa kupiga mikwaju kwenye kundi la  walinzi.Ni kweli  kwamba  hakukamata vizuri na  ukaingia  wavuni na  huenda hilo ni  kosa."

Großbritannien Fußball | Frank Lampard, Trainer Derby County
Frank Lampard kocha wa ChelseaPicha: Reuters/Action Images/T. O'Brien

Kocha wa Manchester United Ole Gunnar Solskjaer  alimueleza  De Gea  kama mtu shupavu  baada  ya  mchezo  huo, lakini  mlinzi wa zamani  wa  klabu  hiyo Phil Neville  alisema  mlinda  mlango  huo hajiamini. Ole Gunnar Solskjaer  alikuwa  na  haya  ya  kusema kuhusu  mlinda  mlango  wake David de Gea baada  ya  kufanya makosa  na  kuizawadia  Chelsea  ushindi  mnono  wa  fainali  ya FA.

"Kila  mmoja  anapaswa kucheza  vizuri  na  kila  mmoja  ana  fursa kila  mara  kucheza  ili kuonesha mchango wake kwa  timu. David anafahamu  alipaswa  kuokoa  goli  la  pili, lakini  imekwisha  tokea. Tunapaswa  kusonga  mbele. Tunapaswa  kuangalia  mbele  kwa  ajili ya  michezo ya  Jumatano. Unaweza  kuona, ni  vigumu  kwa  mlinda mlango  kujisahihisha, mbali  na  David kuokoa kwa ustadi wa hali  ya juu mara  mbili, mara  tatu baadaye."