Lisicki ; Je atairejeshea Ujerumani hadhi ya Tennis?
5 Julai 2013Sabine Lisicki mwenye umri wa miaka 23 mkaazi wa mjini Berlin ameingia fainali baada ya pambano kali dhidi ya Agnieszka Radwanska wa Poland na kumshinda kwa seti 2-1 , kwa 6-4, 2-6 na 9-7.
Lisicki anaingia katika mchezo wake wa kwanza wa mashindano ya Grand Slam leo Jumamosi mchana dhidi ya Mfaransa Marion Bartoli. Mara baada ya ushindi huo wa nusu fainali dhidi ya Radwanska , Lisicki alikiri kuwa haikuwa kazi sahisi kwake.
"Ilikuwa changamoto kubwa kwangu. Nafurahi, kwamba nimeweza kushiriki katika mchezo kama huo na kushinda".
Sabine Lisicki kipenzi hivi sasa cha mashabiki wa mchezo huo katika michuano ya Wimbledon kama ilivyokuwa kwa Steffi Graf katika miaka ya 90 pamoja na Boris Becker.
Maumivu yavuruga mipango yake
Lakini maumivu katika kifundo cha mguu mwaka 2010 pamoja na maradhi ya mzio wa majani yalikaribia kuvuruga ndoto yake ya hata kudiriki kushiriki katika fainali ya Wimbledon.
Maumivu ambayo yalimweka nje kwa miezi mitano na kusababisha kushuka kutoka orodha ya juu ya wachezaji wa tennis duniani hadi kufikia nambari 218, ilimsababishia kuanza kujifunza upya kuingia katika mashindano haya.
Wajerumani kwa mara nyingine tena wanatarajia kutamba tena katika mchezo wa tennis duniani baada ya miaka kadha ya kutamba wakiwa na Steffi Graf.
Bundesliga
Timu za ligi kuu ya Ujerumani Bundesliga zimeanza maandalizi rasmi ya msimu wa mwaka 2013 hadi 14, ambapo mabingwa wa ligi hiyo Bayern Munich wameingia kambini huko Terantino nchini Italia pamoja na kocha wao mpya Pep Guadiola.
Bayern inafungua dimba la ligi hiyo hapo Agosti 9 , itakapopambana na Borussia Moenchengladbach. Makamu bingwa Borussia Dortmund itaingia dimbani siku inayofuata tarehe 10 ikipambana na Augsburg.
Aubameyang mkuki wa Borussia
Wakati huo huo Borussia Dortmund imefanikiwa kupata saini ya mshambuliaji kutoka Gabon Pierre-Emerick Aubameyang ambaye alikuwa anachezea timu ya Saint -Etienne ya Ufaransa. Nayo Arsenal London imethibitisha kuwa Johan Djourou na Francis Coquelin hawatakuwa katika kikosi cha timu hiyo kwa muda wakianzimwa na timu kutoka Ujerumani.
Hamburg SV wameamuazima mlinzi Johan Djourou ambaye alikuwa katika timu ya Hannover 96 pia ya Ujerumani msimu uliopita, na Coquelin anajiunga na Freiburg kwa mkopo.
Nigeria mwishoni mwa juma hili inazindua kampeni ikijaribu kufikia fainali za mashindano ya bara la Afrika kwa mara ya kwanza kwa wachezaji wazaliwa wa nchi za Afrika.
Wapinzani wakubwa wa kimkoa Ghana wamewaondoa Super Eagles , au tai wa kijani kutoka katika michuano ya mwaka 2009 na Niger wakafanya hivyo katika kinyang'anyiro kilichofuata miaka miwili baadaye.
Nigeria yataka kufanya kweli
Lakini Nigeria ambayo ni mabingwa wa kombe la mataifa ya Afrika inatarajiwa kubadilisha mambo mara hii wakati itakapopambana na Cote D'Ivoire katika duru ya kwanza ya mashindano hayo leo jioni kwa fainali itakayofanyika mwaka 2014 nchini Afrika kusini.
Mapambano mengine ni kati ya mabingwa Tunisia dhidi ya Morocco , Senegal inapambana na Mauritania, Mali na Guinea , Burkina Faso na Niger, Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo na Congo Brazzaville, na Burundi na Sudan.
Mwandishi ; Sekione Kitojo / afpe / rtre / afpe
Mhariri: Mohammed Abdul Rahman