1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Klitschko ataka pigano la marudiano na Fury

30 Novemba 2015

Aliyekuwa bingwa wa dunia wa uzani mzito Wladimir Klitschko ameomba waandalizi wa ndondi kumpa nafasi ya kuzichapa tena dhidi ya muingereza Tyson Fury hapo mwakani.

https://p.dw.com/p/1HEuK
Tyson Fury gegen Wladimir Klitschko Boxen
Picha: Reuters/K. Pfaffenbach

Fury mwenye umri wa miaka 27, aliandikisha historia kwa kumzidi nguvu bingwa wa mataji matatu ya uzani wa juu – heavyweight kutoka Ukraine Klitschko kwa wingi wa pointi.

Ushindi huo wa Fury sasa umeweka kikomo udhibiti wa miaka 9 wa Klitschko katika kitengo cha uzani wa juu katika ndondi za kulipwa.

Klitschko sasa ametaka kipengee cha mechi ya marudiano katika mkataba wa pigano hilo kitumike kuhakikisha ndiye anayepata fursa ya kwanza kuzichapa dhidi ya bondia huyo Muingereza.

''japo nilipoteza ulingoni hapo jana ,ninaamini ninauwezo wa kuzichapa ,bado nina hamu ya kupigana'' alisema Klitschko, mwenye umri wa miaka 39. Ameongeza “Bila shaka tutawatangazia lini na wapi tutapigana katika marudio ya ndondi za uzani wa juu''.

Kwa haraka Fury alijibu kwa kusema yuko tayari kupigana na bondia yeyote, ''Nataka kuwa bondia mashuhuri kwa hivyo niko tayari kupigana na mabondia wowote'' ameongeza kusema kuwa ''Bila shaka itakuwa pigano la kukata na shoka''

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Sekione Kitojo