Khodorkovsky apunguziwa kifungo
6 Agosti 2013Mawakili wake wamesema wanakata rufaa dhidi ya uamuzi huo, ambao pia imekubali uamuzi wa mwaka 2010 wa kumpata na hatia. Baba yake Khodorkovsky amesema kuwa amefadhaishwa na hukumu hiyo ambayo ni kinyume na sheria.
Uamuzi huo wa mahakama una maana kwamba Khodorkovsky , ambaye aliwahi kuwa mtu tajiri kabisa nchini Urusi , anatarajiwa kuachiwa huru August , 2014 na mshirika wake Planton Lebedev ataachiwa huru Mei mwaka 2014.
Khodorkovsky na Lebedev walikamatwa mnamo mwaka 2003 na kuhukumiwa mwaka 2005 kwa kukwepa kulipa kodi katika kampuni yao ya Yukos oil katika kesi ambayo ilionekana kwa kiasi kikubwa kuwa ni kulipiza kisasi kwa utawala wa rais Vladimr Putin kutokana na Khodorkovsky kumpa changamoto katika uongozi wake.
Mahakama ya Ulaya
Mwezi uliopita , mahakama kuu ya haki za binadamu ya Ulaya ilitupilia mbali madai kuwa Khodorkovsky alihukumiwa kutokana na sababu za kisiasa katika kesi ya kwanza, lakini ikasema kuwa baadhi ya utaratibu katika kesi hiyo ulikuwa si wa haki.
Kampuni ya Khodorkovsky ya Yukos ilifungwa baada ya kukamatwa kwake, na baadhi ya mali zake zikaangukia katika mikono ya kampuni linalomilikiwa na serikali la Rosneft.
Khodorkovsky na Lebedev walihukumiwa tena katika kesi ya pili mwaka 2010 kwa madai ya wizi wa mafuta kutoka kampuni ya Yukos na kusafirisha fedha walizozipata na kuziingiza katika mtandao wa kibenki.
Desemba mwaka jana mahakama ya mjini Moscow ilipunguza kifungo chao jela kutoka miaka 13 hadi 11.
Ahutubia mahakama
Akihutubia mahakama hiyo kuu kwa njia ya video kutoka katika jela alikofungwa kaskazini magharibi mwa Urusi , Khodorkovsky ameitaka mahakama hiyo kufuta kile alichokiita "uamuzi wa mahakama uliofanywa na watu wasio na elimu."
Amesema kuwa hukumu iliyotolewa mwaka 2010 , ambapo alipatikana na hatia ya kuiba mafuta , inagongana na hukumu ya kwanza ya mahakama hiyo, ambayo ilimpata na hatia ya kutolipa kodi kwa mafuta hayo.
"Hata bado hatuzungumzii hapa utekelezaji wa sheria, lakini kuwapo tayari kuiharibu sheria kama hivi, na hadhi ya mfumo wa sheria, na uaminifu katika taasisi hii ya taifa, kwa ajili tu ya kurefusha kifungo kwa wapinzani wa viongozi wenye mamlaka, Khodorkovsky amesema.
Waungaji mkono wa Khodorkovsky wanahofu kuwa wachunguzi wanajitayarisha kwa madai mengine mapya ili kuendelea kumbakisha jela.
Mwezi Mei , Sergei Guriev , mwanauchumi maarufu mwenye msimamo wa wastani, alikimbia kutoka Urusi akisema anataka kukimbia mbinyo kuhusiana na uchunguzi mpya unaolenga katika ripoti huru ambayo ilikuwa inakosoa hukumu hiyo ya mwaka 2010. Wachunguzi wanadai kuwa waandishi wa ripoti hiyo wameingia katika mzozo wa kimaslahi kwasababu walipokea fedha kutoka kwa Khodorkovsky hapo siku za nyuma.
Mwandishi : Sekione Kitojo / ape
Mhariri: Mohammed Abdul Rahman